In Summary

•Kamanda wa polisi wa kaunti ndogo ya Mwingi kati Peter Mutuma alisema mwili wake ulipatikana ukiwa umelala juu na damu mdomoni na puani.

•"Marehemu alikuwa akilalamika kwa maumivu ya kifua kabla ya kufariki," alisema Mutuma.

Polisi wameanzisha uchunguzi kuhusiana na mauaji ya jamaa mmoja ambaye mwili wake ulipatikana nje ya nyumba yake mapema siku ya Jumanne.

Joseph Kiteme, 33, alipatikana nje ya nyumba yake katika mji wa Mwingi karibu na kituo cha basi.

Kiteme anayetoka eneo la Mui, Mwingi Mashariki alikuwa akifanya kazi ya manamba. Kamanda wa polisi wa kaunti ndogo ya Mwingi kati Peter Mutuma alisema mwili wa marehemu ulipatikana ukiwa umelala juu na damu mdomoni na puani.

 "Marehemu alikuwa amelalamika kuhisi maumivu kifuani kabla ya kufariki," alisema Mutuma. Alisema mwili wake ulihamishwa hadi hospitali ya Mwingi level 4 ukisubiri uchunguzi wa chanzo cha kifo hicho.

Morris Muema, kaka yake mkubwa alisema marehemu alikuwa mtu mtulivu na alishangaa jinsi maisha yake yangeweza kukatishwa kwa ukatili huo.

“Ina maana kuna ukosefu mkubwa wa usalama Mwingi kwa sababu nashindwa kuelewa jinsi kaka yangu aliuawa katikati ya mji,” alidai.

Muema aliongeza kuwa alikuwa na mpango wa kumpeleka kaka yake nyumbani kwa vile afya yake ilikuwa imedhoofika lakini alipofika Mwingi mjini, alikuta maiti yake ikiwa imelala nje ya chumba alichokuwa akiishi.

 

View Comments