In Summary

• Alisema uchunguzi ulifuata, mawasilisho ya mashahidi na matokeo ya uchunguzi kabla na baada ya kuzikwa yalithibitisha kuwa Jeff alikufa eneo la tukio ambapo mwili wake ulipatikana.

• Hii kimsingi iliweka DJ huyo nje ya ghorofa wakati wa kuanguka kwa Jeff.

DJ Faxto anayeshukiwa kwa kifo cha Mwathi
Image: HISANI

Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma Noordin Haji ameeleza ni kwa nini hakuna hata mtu mmoja aliyekamatwa kwa tuhuma za kuhusika na kifo cha mbunifu wa mapambo ya ndani Jeff Mwathi.

Katika barua kwa Mkurugenzi wa upelelezi wa makosa ya jinai (DCI) iliyotiwa saini na mkurugenzi msaidizi wa mashtaka ya umma Gikui Gichuhi, DPP alitaja ushahidi uliowaondolea washukiwa hao mashtaka.

DPP alisema Jeff, ambaye jina lake halisi ni Geoffrey Mwathi Ngugi, alimtembelea DJ Fatxo, jina halisi Lawrence Njuguna Wagura Februari 21 kwa kazi ya usanifu wa mapambo ya ndani katika biashara yake karibu na Eastern Bypass.

Alisema wawili hao pamoja na marafiki wa Jeff walijivinjari kwa chakula na vinywaji katika baa mbalimbali kabla ya kurejea kwa ajili ya mapumziko katika nyumba ya Fatxo saa 3 asubuhi terehe 22 Februari.

Makao hayo yalikuwa kwenye ghorofa ya 10 ya ghorofa ya Redwood ndani ya mtaa wa Roysambu huko Kasarani, Nairobi.

"Iliripotiwa kuwa marehemu alitoweka kwenye chumba cha kulala cha wageni na mwili wake kupatikana kwenye ghorofa ya chini ya jengo hilo," Haji alisema.

Alisema uchunguzi uliofuata, mawasilisho ya mashahidi na matokeo ya uchunguzi kabla na baada ya kuzikwa, yalithibitisha kuwa Jeff alikufa katika eneo la tukio ambapo mwili wake ulipatikana.

Matokeo ya uchunguzi

Haji alisema matokeo ya uchunguzi wa maiti yalionyesha kuwa Jeff alikufa kutokana na kuvuja damu kulikosababishwa na kuanguka kwa kasi kubwa.

Alivunjika viungo, fuvu la kichwa na ubongo wake kutapakaa.

DPP alisema ushahidi wa CCTV ulionyesha DJ Fatxo akiondoka katika nyumba hiyo saa 5.02 asubuhi akiwa na wanawake watatu, kuwapeleka nyumbani Roysambu.

Kamera za CCTV pia ilimnasa Jeff akianguka saa 5.47 asubuhi, kama dakika 45 baada ya Dj Fatxo kuondoka na wageni wake.

Hii kimsingi iliweka DJ huyo nje ya ghorofa wakati wa kuanguka kwa Jeff.

"Picha za CCTV zinaonyesha mwili wa marehemu ukigonga chini na simu yake kutoka kwenye mkono wake wa kulia baada ya kugonga chini.”

DPP alisema CCTV ilinasa kurudi kwa Fatxo kwenye ghorofa saa 9.05 asubuhi ambapo alifahamishwa na walinzi kuhusu kile kilichotokea.

Dakika kumi kabla ya Jeff kuanguka, Haji alisema kamera za CCTV zilinasa binamu ya Fatxo na dereva aliyetambuliwa kama D9 na D8 katika taarifa za mashahidi wakishuka kwenye njia panda saa 5.37 asubuhi wakionekana kumtafuta DJ Fatxo.

Wawili hao pia walinaswa wakipanda njia panda na 5.39am na 5.40am.

 

Wananaswa tena wakitoka kwenye lifti ya ghorofa ya 10 saa 5.47 asubuhi wakirudi ndani ya nyumba, wakati ambapo Jeff alionekana akianguka.

"Hii inawaweka nje ya nyumba wakati wa kifo cha marehemu," DPP alisema.

Haji alisema uchanganuzi wa sampuli za DNA zilizopatikana baada ya uchunguzi wa pili wa maiti uliofanywa na Mwanapatholojia wa Serikali Johansen Oduor kufuatia kufukuliwa kwa mabaki ya Jeff nyumbani kwa mzazi wake huko Laika kaunti ya Nakuru haukuhusisha rafiki yoyote kati ya hao watatu wa kiume na kifo chake.

"Jumla ya maelezo ya mashahidi na ushahidi wa maandishi katika faili hadi sasa unaondoa shaka kwamba kifo cha marehemu kilitokana na kitendo kisicho halali au kutotenda kwa watu watatu wanaohusika na/au kwamba yeyote kati yao walikua na nia ya kumuua Geoffrey Mwathi kinyume cha sheria," DPP alihitimisha.

Hata hivyo, alisema mlango bado uko wazi kwa uchunguzi wa umma kuwasilishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkuu katika Mahakama ya Milimani, Nairobi.

"Kwa wakati huu maelezo katika faili hayafikii kizingiti cha shtaka la mauaji kwa vile uovu haujaanzishwa," Haji alisema.

Muda wa kuwasilishwa kwa uchunguzi huo ulikwisha Mei 23, siku 14 baada ya DPP kutoa tamko hilo na kuondoa shtaka la mauaji.

Mamake Jeff Anne Mwathi ametoa taarifa akisisitiza kuwa mwanawe aliuawa na kumshutumu DCI kwa kuficha uhalifu huo.

"Nimeumia... Walinilazimisha niufukue mwili wa mwanangu na kisha wakaripoti kwamba hakuna ushahidi. Hiyo haikuwa sawa," alisema wakati wa mahojiano Mei 8.

View Comments