In Summary

• Gavana huyo wa zamani alisema kuwa njia pekee ambayo hangeweza kustaafu na Raila ni ikiwa kiongozi wa Azimio angemshawishi vinginevyo.

Naibu kiongozi wa chama cha ODM Wycliff Oparanya, mgombea urais wa ODM Raila Odinga na Gavana wa Mombasa Ali Hassan Joho wakati wa Baraza la Kitaifa la Uongozi katika Bomas Of Kenya mnamo Februari 25,2022.
Image: ENOS TECHE

Gavana wa zamani wa Mombasa na ambaye ni naibu kinara wa ODM, Ali Hassan Joho amedokeza mpango wake kuhusu mustakabli wake wa kisiasa.

Akizungumza katika kaunti ya Migori siku mbili zilizopita, Joho alidokeza kwamba nia yake ni kustaafu siasa pindi kiongozi wa chama hicho, Raila Odinga atakapostaafu.

Joho alisema kwamba yeye ni mwanachama wa kudumu wa ODM na katika maisha yake yote ya kisiasa, alianza na ODM na kama mwanafunzi mtiifu wa Odinga, atastaafu siasa pamoja na yeye.

Gavana huyo wa zamani alisema kuwa njia pekee ambayo hangeweza kustaafu na Raila ni ikiwa kiongozi wa Azimio angemshawishi vinginevyo.

"Mimi ni mwanachama mwanzilishi wa Orange Democratic Movement (ODM) na ninataka kuwaambia, katika maisha yangu ya kisiasa isipokuwa Raila atasema vinginevyo, niliingia katika siasa na Raila na nitaondoka na Raila," Joho alisema.

Huku gavana huyo wa zamani wa Mombasa akielezea utayari wake wa kujiondoa katika siasa pamoja na Raila, alisalia na matumaini kuwa ODM itaunda serikali itakayomrithi 2027.

Hata hivyo, Joho hakusema ikiwa kustaafu kutoka kwa siasa ndio utakuwa mwisho wa azma yake ya urais.

Matamshi yake yaliibuka wakati viongozi wengi katika ODM wakilenga kuchukua wadhifa wa kiongozi wa chama kutoka kwa Raila.

Alijiunga na siasa za kitaifa kwa mara ya kwanza 2007 kama Mbunge wa Kisauni, kabla ya kuchaguliwa kuwa gavana katika chaguzi za 2013 na 2017.

View Comments