In Summary

• Kindiki, Duale na Tuya wamehifadhi hati zao za awali ingawa Chirchir amehamishwa. Hapo awali alishikilia hati ya Nishati.

• Rebecca Miano ambaye alikuwa Waziri wa zamani wa Viwanda na Biashara ameteuliwa kwa wadhifa wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

SENETA THANG'WA
Image: HISANI

Seneta wa Kiambu Karungo Wa Thang'wa amewaambia wabunge kuwa waangalifu wanapokagua mawaziri wapya walioteuliwa.

Thang'wa alisisitiza umuhimu wa wabunge hao kuzingatia maoni ya Wakenya kabla ya kupendekeza yeyote kati ya walioteuliwa na rais Ruto Ijumaa alasiri.

“Sasa ni wajibu wa wabunge, kabla hawajaidhinisha mtu yeyote wawasikilize wananchi,” alisema.

Akizungumza Jumamosi eneo la Mwea, Kirinyaga, seneta huyo alibainisha kuwa hiyo ndiyo njia pekee ya kuepuka maandamano jinsi ilivyoshuhudiwa hivi majuzi kote nchini.

Alikuwa miongoni mwa viongozi walioandamana na Naibu Rais Rigathi Gachagua kwa kuwekwa wakfu na kumweka wakfu Askofu wa eneo la Kirinyaga Samuel Karimi.

Gavana Ann Waiguru hakuhusika katika hafla hiyo.

"Raia wakisema hivi, msitake tuseme kataa, wakisema kataa huyo, mnareject. Wakenya ni milioni 50,” alisema.

Alisema wapo watu wengi wanaostahili ambao wanaweza kuchukuliwa nafasi hizo. Hata hivyo, aliwaomba wakazi wa Mlima Kenya kuwaombea wale kutoka eneo hilo ambao wameteuliwa.

Rais William Ruto aliteua Ijumaa mawaziri 11 baada ya kuvunja baraza la mawaziri mnamo Julai 11 kufuatia maandamano yaliyokithiri ya Jenerali Z nchini.

Alisema kundi la kwanza la wateule wa Baraza la Mawaziri litamsaidia katika kuendesha mageuzi yanayohitajika kwa haraka na yasiyoweza kutenduliwa nchini.

Mawaziri sita waliorejea ni Kithure Kindiki (Mambo ya Ndani) Alice Wahome (Ardhi, Kazi za Umma, Maendeleo ya Miji na Makazi) Aden Duale (Ulinzi) Davis Chirchir (Barabara), Soipan Tuya (Mazingira).

Kindiki, Duale na Tuya wamehifadhi hati zao za awali ingawa Chirchir amehamishwa. Hapo awali alishikilia hati ya Nishati.

Rebecca Miano ambaye alikuwa Waziri wa zamani wa Viwanda na Biashara ameteuliwa kwa wadhifa wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

"Mashauriano zaidi yanaendelea na baada ya hapo nitatangaza majina zaidi kwa wakati ufaao," Ruto alisema.

Ruto anatazamiwa kupeleka majina ya waliopendekezwa bungeni ili kuhakikiwa. Wabunge kwa sasa wako mapumzikoni na wanatazamiwa kurejea wiki ijayo.

View Comments