In Summary

•Naibu gavana wa Machakos alidai kuwa Raila   yafaa ajitokeze kwa  uwazi na kukubali kuathiri demokrasia kinyume na itikadi zake alizojitangaza hapo awali.

•Hata hivyo alisifia viongozi ambao wameshikilia msimamo wa kutojiunga na serikali ya Kenya Kwanza kama vile Kalonzo Musyoka.

RAILA ODINGA
Image: EZEKIEL AMING'A

Kiongozi wa ODM Raila Odinga amehimizwa kueleza wazi madai yake ya kuhusishwa na utawala wa Kenya Kwanza.

Naibu Gavana wa Machakos Francis Mwangangi, alisema wakenya wengi wamejawa na maswali mengi kuhusu jinsi Raila alikuwa akicheza mchezo wa paka na panya kuhusu suala hilo.

Akishiriki  ibaada  katika kanisa la Kariobangi AIC katika mji wa Machakos, naibu Gavana huyo alisema waziri mkuu huyo wa zamani anafaa kujitokeza wazi na kukubali kuathiri demokrasia kinyume na itikadi zake alizojitangaza hapo awali.

"Iwapo atakubali au la itaingia katika vitabu vya historia kwamba kiongozi wa chama cha ODM alikuwa amevuruga demokrasia kwa kukubali kuua upinzani katika nchi yake kwa kukubali kwenda kulala na serikali" alisema.

Aidha,aliwasifu viongozi waliosalia  wa Azimio kama Kalonzo, Wamalwa, Martha Karua na Kioni ambao walieka msimamo wao sawa wa kutowasaliti wakenya kwa kujiunga na serikali ya Kenya Kwanza.

Vile vile alimtaka Kalonzo kutolegea bali kuongoza kikosi kilichosalia cha Azimio kuwaokoa wakenya kutoka kwa utawala wa sasa wa muungano huo.

Siku chache zilizopita,Raila alikuwa ametoa kauli kwa kudai kuwa chama chake cha ODM hakijaungana na serikali ya Kenya Kwanza.

"Kama ilivyobainishwa katika taarifa yetu ya Jumanne, Julai 23, 2024, si Chama cha ODM wala Azimio la Umoja One Kenya Coalition Party ambayo imeingia katika makubaliano yoyote ya muungano na chama cha UDA cha Rais Ruto." Raila alisema.

View Comments