In Summary

• Awali Salasya alitangaza kuwa anatafuta mwanamke wa kumuoa.

• Natafuta tu mwanamke mwenye maombi sana, msichana mdogo sana, msichana makini, msichana anayetegemewa - Salasya.

Video ya mbunge wa Mugirango Kusini Slyvanus Osoro akitoa ushauri kwa wabunge wapya Linet Chepkorir maarufu Toto na Peter Salasya imezua maoni kinzani kwenye mitandao ya kijamii.

Katika video hiyo, Osoro ambaye ni kiranja wa waliowengi katika bunge la kitaifa alionekana akiwapa ushauri wawili hao kuoana na kupata watoto katika kile kilichoonekana kama ni mzaha.

Linet Toto ni mwakilishi wa kike katika kaunti ya Bomet huku Peter Salasya akiwa mbunge wa Mumias East, wote ni wanasiasa ambao walichaguliwa kwa mara ya kwanza kabisa katika uchaguzi mkuu uliopita wa Agosti 9.

“Hii ndoa ikuwe sawa, hii ndio tumeshikanisha. Wewe ndio bwana Salasya, na wewe Toto ndio bibi, ingia hapa kabisa. Mzae watoto wewe Salasya ni mweupe, Toto ni mweusi, mtoto awe Mhindi, maisha ni namna hiyo,” Osoro alionekana akiwashauri hao wawili hao huku wenzao wakicheka.

Kwa muda mrefu, mbunge Salasya amekuwa akitangaza kuwa anatafuta mke wa kuoa huku baadhi ya wabunge wa kutoka Magharibi wakiunda kamati ya kumtafutia mwanamke wa matakwa yake.

“Natafuta tu mwanamke mwenye maombi sana, msichana mdogo sana, msichana makini, msichana anayetegemewa, anayeonekana na lazima awe na uwezo wa kuzungumza na watu wa mashambani. Uko tayari kuungana nami twende kutafuta kura? Mimi ni mtu wazi. Kwani naeza pelekwa pelekwa hivi. Mimi ni mbunge na unajua nimewaaminisha watu kuwa mimi ni mtu mwenye akili sana. Nina nguvu,” Salasya alinukuliwa katika mahojiano na Standard.

View Comments