In Summary

• Charity alikuwa miongoni mwa wanafunzi wanne waliofariki papo hapo. Wengine wanne walifariki walipokuwa wakipokea matibabu katika hospitali walikokuwa wamekimbizwa.

• Jumla ya wasichana sita na wavulana wawili wenye umri kati ya miaka tisa na kumi na mbili walifariki katika ajali hiyo.

Wanafunzi watano, dereva waliaga katika ajali iliyotokea Kaberengu siku ya Jumamosi, Juni 24.
Image: HISANI

Zikiwa ni takribani wiki mbili tangu majonzi kugubika wazazi nchini kufuatia ajali mbaya ya barabarani iliyohusisha basi la shule ya Ebenezer kwenye barabara kuu ya Webuye kwenda Eldoret, baadhi ya familia zimekuwa zikiendesha shughuli za maziko ya malaiko hao walioangamia.

Mkasa wa ajali hiyo uliwaua watoto 8 wa shule hiyo na sasa imebainika kwamba mmoja wa watoto walioangamia katika ajali hiyo ndio mwanzo alikuwa ameshinda udhamini wa masomo kwenda Marekani.

Kwa mujibu wa taarifa zilizokusanywa na Citizen, wazazi wa msichana huyo wa miaka 9, Charity Kate Oor, ilisema kuwa msichana wao kabla ya mkasa alkuwa ameanza maandalizi ya kuhamia USA aliposhinda udhamini wa masomo yake.

Kulingana na babake Bw. Marcus Oor, alikuwa na miadi ya Visa katika ubalozi wa Marekani jijini Nairobi Jumatano hii, Julai 5, 2023.

"Nilipaswa kuchukua visa yangu na ya binti yangu ili kuturuhusu kusafiri hadi Marekani, lakini hapa ninamzika mtoto wangu," alisema Oor siku ya Jumatatu katika hafla ya maziko ya bintiye.

“Inaumiza moyo wangu. Ninajiuliza kwa nini hii ilibidi kutokea?"

Marcus pamoja na mkewe Lilian Oor walimsifu binti yao kama mtoto mwenye akili, nidhamu na mchapakazi.

Wanafunzi hao walikuwa wakitoka katika ziara ya kimasomo ya shule mjini Eldoret mnamo Juni 24 wakati lori lilipogonga basi lao la shule kwa nyuma.

Charity alikuwa miongoni mwa wanafunzi wanne waliofariki papo hapo. Wengine wanne walifariki walipokuwa wakipokea matibabu katika hospitali walikokuwa wamekimbizwa.

Jumla ya wasichana sita na wavulana wawili wenye umri kati ya miaka tisa na kumi na mbili walifariki katika ajali hiyo.

View Comments