In Summary

•Karen Nyamu ameibua malalamishi kuhusu uamuzi wa seneti wa kuunga mkono kubanduliwa kwa gavana Kawira Mwangaza.

•Pia alimkosoa Kawira Mwangaza kwa kutokuwa na uwezo wa kudhibiti viongozi wengine wa kaunti ya Meru.

KAREN NYAMU
Image: FACEBOOK

Seneta wa kuteuliwa Karen Nyamu ameibua malalamishi kuhusu uamuzi wa seneti wa kuunga mkono kubanduliwa kwa gavana Kawira Mwangaza.

Usiku wa kuamkia Jumatano, seneti iliidhinisha kutimuliwa kwa gavanahuyo wa kaunti ya Meru baada ya maseneta kupiga kura kukubaliana na mashtaka aliyokuwa akikabiliana nayo.

Katika taarifa yake Jumatano asubuhi, seneta Karen Nyamu alibainisha kuwa kiwango cha kumtimua Kawira Mwangaza kilikosa kufikiwa kwa kiasi kikubwa na kulikuwa na sababu dhaifu sana za kuunga mkono mashtaka hayo.

"Misingi dhaifu sana ya kuunga mkono kubanduliwa. Kiwango kilikosekana kwa mbali. Hata hivyo, ilibidi uamuzi wa kisiasa ufanywe ili kuokoa Meru kutokana na vuta nikuvute,” Seneta Karen Nyamu alisema kupitia ukurasa wake wa Facebook.

Seneta huyo wa kuteuliwa hata hivyo pia alimkosoa Kawira Mwangaza kwa kutokuwa na uwezo wa kudhibiti viongozi wengine wa kaunti ya Meru.

“Vipi huna uwezo wa kushughulika na watu wako. Ukiwa gavana, ulikuwa mwanasiasa mkuu zaidi Meru. Unapaswa kuwa wewe ndiye unayefanya unyanyasaji, na sio kulalamika juu yake, " alisema.

Aliongeza, "Yote kwa yote ni siku ya huzuni. Kutoka G7 hadi G6? Ni uchungu.’

Mwangaza alipoteza kiti chake usiku wa kuamkia Jumatano baada ya maseneta kuunga mkono kutimuliwa kwake na bunge la kaunti ya Meru.

Maseneta 26 walipiga kura kuunga mkono shtaka la kwanza la ukiukaji mkubwa wa katiba na sheria zingine.

Maseneta 14 walikosa kupiga kura huku wanne wakipiga kura kumuunga mkono.

Katika shtaka la pili la utovu wa nidhamu uliokithiri, maseneta 26 walipiga kura ya kuunga mkono kushtakiwa kwake, wawili walipinga, huku wengine 14 wakikosa kupiga kura.

Maseneta 27 waliunga mkono shtaka la matumizi mabaya ya afisi, kura moja ya kumuunga mkono na 14 hawakupiga kura.

Wengi wa waliokosa kupiga kura ni washirika wa vyama vya Upinzani.

“Kulingana na Kifungu cha 181 cha Katiba, Kifungu cha 33 cha Sheria ya Serikali ya Kaunti na Kanuni ya Kudumu ya 86 ya Kanuni za Kudumu za Seneti, Seneti imeazimia kumuondoa afisini kwa kumwondoa madarakani Mhe. Kawira Mwangaza, Gavana wa Kaunti ya Meru na gavana huyo kukoma ipasavyo. kushika wadhifa huo," Spika Amason Kingi alisema.

Hii ilikuwa ni mara ya tatu kwa Mwangaza kung'olewa madarakanina  kufikishwa katika seneti, tangu alipochaguliwa kuwa wadhifa wake Agosti 2022.

View Comments