Kaimu Jaji mkuu Philomena Mwilu

Kaimu Jaji mkuu Philomena Mwilu ataendelea kushikilia nafasi hiyo hadi pale jaji mkuu wa kudumu atakapoteuliwa kujaza nafasi ya David Maraga aliyestaafu siku ya Jumatatu.

Mahakama kuu siku ya Jumanne ilitupilia mbali ombi la mwanaharapkati Okiya Omtata kumzuia Mwilu kuhudumu katika wadhifa huo.

Maraga alimpokeza Mwilu mamlaka hayo siku ya Jumatatu na atatekeleza majukumu ya jaji mkuu hadi pale tume ya huduma kwa mahakama itapojaza nafasi hiyo.

Jaji Antony Mrima aliamuru kwamba ombi la Omtata lilikuwa la mapema na lilihitaji kusikizwa kikamilifu kabla ya mahakama kufanya uamuzi wake.

Omtata alikuwa ameshikilia kwamba Mwilu hawezi kuhudumu katika ofisi ya jaji mkuu kutokana na kesi inayolenga kuondolewa kwake ofisini na ambayo iliwasilishwa kwa JSC.

"Kwa upande mmoja Omtatah anashikilia msimamo kwamba Mwilu hapaswi kuhudumu katika nafasi hiyo kwa sababu maadili yake yametiliwa shaka, kwa upande mwingine, Mwilu anasisitiza kwamba hakuna uamuzi wowote uliyotolewa kuonyesha kama ana hatia," jaji alisema.

Jaji alisema kuwa Mwilu anapaswa kudhaniwa kuwa hana hatia hadi pale madai dhidi yake yatakathibitishwa na uamuzi kufanywa na kwa hivyo haitakuwa haki kukubali ombi la Omtata kabla ya uamuzi kutolewa.

Jaji Mrima aliamuru kwamba kesi hiyo itajwe Februari 17.

Omtata anataka Mwilu kusubiri hadi pale tume ya huduma kwa mahakama (JSC) itakaposikiza na kumuondolea lawana kwa madai ya ufisadi na matumizi mabaya ya mamlaka dhidi yake.

Anataka mahakama kufutilia mbali barua iliyoandikwa na aliyekuwa jaji mkuu David Maraga akimteua Mwilu kuhudumu kama kaimu Jaji Mkuu.

View Comments