In Summary

• Familia hiyo iliandikisha taarifa katika kituo cha polisi cha Rabai.

• Kamanda wa polisi katika eneo la Rabai, Fred Abuga alisema kuwa hawajafanikiwa kupata mwili huo bado.

Kaburi aliyokuwa amezikwa Bi Mwero
Image: The Star

Familia moja kutoka Mazeras kaunti ya Kilifi imepigwa na butwaa baada ya watu wasiojulikana kufukua mwili wa mtu ambaye walizika miezi minne iliyopita.

Mwili huo unadaiwa kufukuliwa usiku wa Jumatatu.

Daniel Lwambi, 77, alisema kuwa alizika bibi yake Fatuma Mwero mnamo tarehe 27 mwezi Februari.

Asubuhi ya kuamkia Jumanne aliarifiwa kuwa wanakijiji walipata kaburi likiwa wazi na jeneza pamoja na mwili vimeondolewa.

Lwambi alieleza kuwa wanashuku kuwa huenda tukio hilo lilisababishwa na mgogoro wa ardhi kati ya familia na jamaa mmoja mwenye asili ya kiarabu aliyedai kuwa kipande cha ardhi ambapo alizikwa Mwero ni chake.

Familia hiyo ambayo inaishi kwenye kipande kingine cha ardhi iliandikisha taarifa katika kituo cha polisi cha Rabai.

Kamanda wa polisi katika eneo la Rabai, Fred Abuga alisema kuwa hawajafanikiwa kupata mwili huo bado.

Abuga alisema kwamba kulikuwa na mzozo kuhusu kipande hicho cha ardhi kwa muda mrefu.

Jirani yao alipata amri ya korti ya kusimamisha mazishi ila familia hiyo ikaendelea kuzika Mwero pale. Jirani huyo alienda tena mahakamani ila hatujapokea taarifa nyingine kutoka kortini” Abuga alisema.

Kwa upande wake Bw. Lwambi alisema kuwa amri ya korti ilikuwa ya kuzuia maendeleo yoyote kufanyiwa kwenye kipande hicho cha ardhi.

Shamba hili lilimilikiwa na mzungu aliyeenda baada ya nchi kupata uhuru. Tuliandikisha kupitia mahakama kupatiwa kipande hiki cha ardhi na tukaruhusiwa na mrithi wake anayeishi Uingereza kukimiliki. Tajiri yule alileta nambari ghushi kutoka mahala pengine ili kudai umiliki wa shamba hili” Bw Lwambi alisema.

Familia hiyo imekuwa ikiishi kwenye shamba hilo tangu 1960.

Bi Mwero alikuwa mtu mzima wa kwanza kuzikwa pale baada ya watoto watatu kuzikwa pale miaka mingi iliyopita.

(Mhariri Davis Ojiambo)

View Comments