In Summary

• Matamshi ya Ruto yanajiri wakati Rais amekosolewa kwa kukataa kuteua majaji sita ambao Ikulu inasisitiza wana maswali kuhusu maadili yao.

• DP alisema viongozi lazima wazingatie sheria na waache kushinikiza marekebisho ya Katiba kwa ajili ya matakwa yao ya kibinafsi.

William Ruto Naibu rais William Ruto akizungumza katika kanisa la House of Hope mtaani Kayole siku ya Jumapili, Januari 10, 2021.
Image: DPPS

Taarifa ya Gideon Keter

Naibu Rais William Ruto amewaambia wale walio madarakani kufanya kazi kwa mujibu wa sheria katika ujumbe ambao ulionekana kumlenga, Rais Uhuru Kenyatta.

"Kila mtu aliyepewa jukumu la uongozi lazima afanye kazi kwa kufuata sheria na afuate Katiba,"

Ruto alisema alipokutana na viongozi wa kisiasa, dini na jamii kutoka ngome ya Uhuru, Kiambu.

Viongozi waliokuwepo wakati wa mkutano huo ni pamoja na wabunge Moses Kuria (Gatundu Kusini), Kimani Ichung’wa (Kikuyu), Rigathi Gachagua (Mathira) na George Kariuki (Ndia).

Matamshi ya Ruto yanajiri wakati Rais amekosolewa kwa kukataa kuteua majaji sita ambao Ikulu inasisitiza wana maswali kuhusu maadili yao.

DP alisema viongozi lazima wazingatie sheria na waache kushinikiza marekebisho ya Katiba kwa ajili ya matakwa yao ya kibinafsi.

Alisema pale ambapo masilahi ya wale walio madarakani yanakinzana na Katiba, ni matakwa ya viongozi ambayo lazima yalinganishwe na sheria na sio kinyume chake.

“Nguvu inayotolewa na Wakenya na inayotekelezwa na viongozi inapaswa kuwa katika kufuata sheria. Kuna wale ambao bado wanaamini kuwa ikiwa matakwa yao yanakinzana na Katiba, basi Katiba inapaswa kubadilishwa ili iwe sawa na ajenda zao, ”Ruto alisema katika makazi yake rasmi ya Karen siku ya Alhamisi.

"Ikiwa matakwa yako yanakinzana na Katiba, ni matakwa yanayofaa kubadilishwa sio Katiba inayobadilishwa ili kutoshea masilahi ya kibinafsi ya mtu."

Wakati wa sherehe za Siku ya Madaraka huko Kisumu, Ruto pia alishikilia msimamo kuwa taasisi za serikali zinafaa kuheshimiwa.

Alitaka "Bunge imara, serikali thabiti na Mahakama huru".

Aliendelea: "kitakuwa kitendo cha usaliti mkubwa ikiwa tutaruhusu ushabiki wa kikabila na ibada za utu kuharibu msingi thabiti wa ukatiba na utawala wa sheria katika taifa letu."

Rais Uhuru na mshirikishi wake mkuu katika mchakato wa BBI Raila Odinga wanataka kurekebisha Katiba ya 2010, mchakato ambao Mahakama Kuu imetangaza kuwa ni kinyume cha katiba.

Uhuru na Raila tangu wakati huo wamekata rufaa juu ya uamuzi huo na kesi hiyo imepangwa kusikilizwa katika Korti ya Rufaa mwishoni mwa mwezi huu.

Wakati wa sherehe za Siku ya Madaraka huko Kisumu, Rais alikosoa jopo la majaji watano wa Mahakama Kuu kwa uamuzi dhidi ya mchakato wa BBI, akisema marekebisho ambayo pamoja na mambo mengine yanaweza kuona kupanuka kwa serikali na Bunge yote ni kwa faida ya nchi.

View Comments