HABARI NA GEORGE OWITI;
Watu wawili wamekufa papo hapo na mwingine alitoroka bila kujeruhiwa baada ya gari la kibinafsi walilokuwa wakisafiria kupigwa risasi kando ya barabara ya Nairobi- Machakos katika eneo la Kathome katika Kaunti ya Machakos.
Kamishna wa Kaunti ya Machakos John Ondego alisema gari hilo la Honda Vitz lilikuwa na abiria watatu wakati tukio hilo lilitokea Ijumaa.
Ondego alisema walishambuliwa na wauaji ambao waliwafuata kutoka kituo cha ununuzi cha Kyumbi karibu na barabara kuu ya Nairobi - Mombasa.
Ondego alisema mmoja wa wahasiriwa alikuwa afisa wa polisi aliye katika kaunti ndogo ya Mwala.
Alisema watatu hao walikuwa wakionekana katika rada yao ya wauaji ambao walizuia gari lao kufikia eneo la uhalifu.
"Mmoja wao ni afisa wetu wa Mwala na inaonekana walikuwa wakifuatwa kutoka nyuma kwa sababu watu wenye bunduki walikuwa wakiwafuata kwa nyuma. Kwa kweli hatujui sababu ya shambulio hilo" Ondego alisema.