In Summary

• Waliofariki ni pamoja na mkewe, majirani na waendesha bodaboda ambao walikuwa wamekimbilia nyumbani kwake kuangalia kilichokuwa kinafanyika baada kusikia milio ya risasi Jumanne asubuhi.

• Watu wengine wawili walipigwa risasi na kujeruhiwa vibaya na wamelazwa katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta.

• Hili ni tukio la hivi punde kutokea katika msururu wa visa vya mauaji vinavyo husisha maafisa wa polisi.

Tukio hilo baadaye lilizua maandamano katika barabara ya Thiongo huku wenyeji wakidai majibu kuhusu mauaji hayo.
Image: Enos Teche

Afisa wa polisi aliwapiga risasi na kuwaua watu sita kabla ya kujitoa uhai katika eneo la Kabete Nairobi katika kisa cha kushangaza.

Waliofariki ni pamoja na mkewe, majirani na waendesha bodaboda ambao walikuwa wamekimbilia nyumbani kwake kuangalia kilichojiri waliposikia milio ya risasi Jumanne asubuhi.

Polisi walisema konstebo Benson Imbatu aliyekuwa akihudumu katika kituo cha polisi cha Kabete alienda nyumbani akiwa na bunduki yake aina ya AK47 na kuzua ugomvi na mkewe Carol Imbatu.

Mzozo baina yao ulibadilika kuwa mauti.

Majirani na waendesha bodaboda wanaohudumu karibu na Heights Apartment alikokuwa afisa huyo walikimbilia kwenye nyumba hiyo kuangalia kilichokuwa kikiendelea.

Hii ilikuwa baada ya wao pia kuona moto ukitoka kwenye nyumba hiyo, polisi walisema.

Na katika patashika hiyo, afisa huyo wa polisi alitoka nje akiwa na bunduki na kuanza kuwamiminia risasi watu waliokuwa nje ambapo aliua watu watano wakiwemo waendesha bodaboda wawili na majirani wake.

Image: Enos Teche

"Aliendelea kufyatua risasi akiwafukuza watu hata waliokuwa mbali na nyumba yake," alisema jirani Jane Wanjiru aliyejificha nyumbani kwake.

Watu wengine wawili walipigwa risasi na kujeruhiwa vibaya na wamelazwa katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta.

Polisi walioitwa kwenye eneo la tukio waliizingira nyumba hiyo kabla ya kusikia mlio wa risasi na baadaye kugundua kuwa alijiua kwa kujipiga risasi shingoni.

Mkuu wa polisi wa Dagorreti Francis Wahome alisema wanandoa hao walikaa peke yao kwenye nyumba hiyo.

"Hatujui nia ya tukio hilo lakini tumepoteza watu saba akiwemo afisa aliyefariki kwa kujitoa uhai," alisema Wahome.

Image: Enos Teche

Hili ni tukio la hivi punde kutokea katika msururu wa visa vya mauaji vinavyo husisha maafisa wa polisi.

Tukio hilo limezua maandamano katika eneo hilo huku wahudumu wa bodaboda wakifunga barabara na kuasha moto. 

View Comments