KFC yakosa Viazi vya kupika chipsi, wateja wapewa ugali
Siku ya Jumatatu duka la vyakula vya haraka, Kentunky Fried Chicken (KFC) lilitangaza kuishiwa na viazi vya kupika vibanzi au chipsi
Katika taarifa, KFC ilisema kuwa Wakenya walikula sana vibanzi (chipsi) msimu wa sherehe, na sasa wameishiwa na viazi.
Vibanzi ni moja wapo wa vyakula vinavyopendwa na wengi nchini Kenya hasa katika maeneo ya mijini. KFC katika taarifa iliomba wateja kuagiza vyakula mbadala kuandamana na kuku. Hii ni kufuatia uhaba wa viazi unaoshuhudiwa katika maeneo yote.
Baadhi ya vyakula wateja waliombwa kuagiza ni Ugali na Mandazi,
"Familia ilikuwa kweli Desemba yenye furaha. Mlikula sherehe na mapochopocho ya KFC. Nyinyi nyote mlipenda chipsi zetu sana..na tumeishiwa viazi. Poleni! Wahudumu wetu wanajitahidi kusuluhisha suala hilo."
Uzalishaji wa viazi umepungua kwa kiasi kikubwa huku nchi nyingi zikiripoti uhaba mwezi Desemba 2021. Marekani, Japan na Afrika Kusini ni miongoni mwa nchi zilizoripoti uhaba huo wa viazi. Kulingana na Business Daily, Mkurugenzi Mtendaji wa KFC Afrika Mashariki, Jacques Theunissen anahusisha uhaba huo na ucheleweshaji usafirishaji kutokana na janga la Covid-19.