In Summary

•Watatu hao walikuwa wamevamia mwanamke mmoja aliyekuwa anatembea kuelekea nyumbani kabla yake kupiga kelele iliyovutia waendesha bodaboda  waliokuwa karibu na eneo hilo la tukio.

•Maafisa kutoka kituo cha Kinoo waliweza kufika katika eneo la tukio na kuwanusuru washukiwa hao ambao walipatikana na  bunduki ya kujitengenezea iliyo na uwezo wa kupiga risasi.

crime scene 1
Image: HISANI

Jamaa watatu wanaendelea kupokea matibabu maalum katika hospitali ya Kiambu baada ya kushambuliwa na umati wenye ghadabu katika eneo la Kinoo, kaunti ya Kiambu usiku wa Jumapili.

Kelvin Kamau, Erick Karanja na Topla Muteti walinusurika kifo kwa tundu la sindano baada ya maafisa wa polisi kuwaokoa kutoka kwenye umati wa waendesha bodaboda na raia wengine ambao walikuwa tayari kukatiza maisha yao.

Kitengo cha Upelelezi wa jinai (DCI)  kimeripoti kwamba watatu hao walikuwa wamevamia mwanamke mmoja aliyekuwa anatembea kuelekea nyumbani kabla yake kupiga kelele iliyovutia waendesha bodaboda  waliokuwa karibu na eneo hilo la tukio.

Watatu hao walifanikiwa kuiba vitu kadha kutoka kwa mwanamke huyo na kutoroka kwa pikipiki ila waendesha bodaboda zaidi ya 30 wakawafuata nyuma na kuwafikia walipokuwa wanakaribia kituo cha magari cha 87.

Baada ya kuona wamefikiwa washukiwa walijaribu kuruka kutoka kwa pikipiki na kutoroka ila wakaanguka kwa kishindo. 

Waendesha bodaboda wale waliwazingira na kuwashambulia kwa mateke na mangumi  huku wakiwashtumu kwa kuwaharibia jina kutokana na hatua yao ya kutumia pikipiki kutekeleza uhalifu.

Maafisa kutoka kituo cha Kinoo waliweza kufika katika eneo la tukio na kuwanusuru washukiwa hao ambao walipatikana na  bunduki ya kujitengenezea iliyo na uwezo wa kupiga risasi.

Washukiwa wanaendelea kuhudumiwa hospitalini wakiwa katika hali mahututi huku pikipiki waliyokuwa wanatumia ikizuiliwa katika kituo cha polisi cha Kinoo.

View Comments