In Summary
  • Mwalimu afikishwa mahakamani kwa kuandika ujumbe Facebook akidai kuwa bosi wa TSC Nancy Macharia amefariki
Image: Douglas Okiddy

Mwalimu wa kiume ambaye aliandika ujumbe kwenye mtandao wa kijamii wa Facebook akidai kuwa bosi wa TSC Nancy Macharia amefariki amefunguliwa mashtaka ya unyanyasaji mitandaoni.

Jeremiah Mwavuganga Samuel, 31, mwalimu wa Shule ya Msingi ya Musiini huko Makueni Jumanne alifikishwa mbele ya mahakama ya Milimani na kukanusha shtaka la unyanyasaji wa mtandao.

Mwavuganga pia alikana shtaka la pili la kuchapisha taarifa za uongo.

Inadaiwa kuwa katika tarehe tofauti kati ya Januari 16 na 20 mwaka huu, kwa pamoja na wengine ambao hawakufika mahakamani, kwa kutumia akaunti yake ya Facebook aliandika madai ya uongo dhidi ya Macharia ambayo yanadaiwa kulenga kumtia hofu.

Aliandika “Breaking news Nancy Macharia AMEFARIKI, mwili wake umepatikana kwenye kitanda cha Oyuu. Inadaiwa kuwa Oyuu alimuua  baada ya kukosa kumbusu. RIP Macharia… ooh ilikuwa ndoto tu. Na iwe hivyo,”

Alikanusha mashtaka na kuiomba mahakama kumpa masharti ya dhamana.

Hakimu Mkuu Susan Shitubi amwachilia kwa bondi ya Sh 650,000 au dhamana mbadala ya pesa taslimu Sh 100,000.

Mwalimu huyo alikamatwa wikendi katika Kituo cha Ununuzi cha Makutano huko Nzaui, Makueni.

Ripoti za polisi zinadai kwamba alipokamatwa alipatikana akiwa na simu ambayo ilitumiwa kuunda chapisho la virusi kuhusu kifo cha Macharia.

Kulingana na polisi, Macharia ambaye alitoa ripoti hiyo alisema uchapishaji huo ulikuwa na nia mbaya ulisababisha hofu, hofu kwa familia yake na kwamba uliharibu sifa na uadilifu wake kama mtumishi wa umma.

Kesi hiyo itatajwa Februari 8.

 

 

 

 

 

View Comments