In Summary

•Whitney Atieno, 19, aliuawa Jumapili kwa kupigwa risasi nje ya saluni ambako alikuwa ameenda kusuka nywele zake kwa ajili ya shule.

•Whitney alikuwa mwanafunzi wa kidato cha nne katika Shule ya Sekondari ya Nakuru Central.

Bunduki
Image: Andrew Kasuku

IPOA imeanza uchunguzi kuhusu tukio la mauaji ya risasi ya mwanafunzi wa kidato cha nne katika mtaa wa Lakeview, kaunti ya Nakuru.

Whitney Atieno, 19, aliuawa Jumapili kwa kupigwa risasi nje ya saluni ambako alikuwa ameenda kusuka nywele zake kwa ajili ya shule.

Alikuwa pamoja na rafiki yake mwenye umri wa miaka 18 walipodaiwa kupigwa risasi na polisi wakati wa msako dhidi ya genge la wahalifu.

"Kulingana na ripoti za mara moja kuwa polisi walihusika, Mamlaka ilituma Timu kwa lengo la kuchunguza zaidi tukio hilo," mwenyekiti wa IPOA Anne Makori alisema katika taarifa yake ya Jumanne.

Wasichana hao walikuwa wametoka nje ya saluni kuangalia baada ya kusikia zogo walipopigwa risasi. Whitney alikufa papo hapo lakini rafiki yake, Ruth, akajeruhiwa vibaya.

Makori alisema timu hiyo imewahoji baadhi ya mashahidi na kuwasiliana na polisi wakiwemo makamanda, pamoja na taratibu nyingine za upelelezi.

Alisema, hii inalenga kupata habari na nyenzo muhimu ili kutatua mazingira yanayozunguka tukio hilo.

"Tumezungumza na baadhi ya wanafamilia na kuwapa rambirambi marafiki zao na watu wengine ambao wameathirika," Makori alisema.

"Pale ambapo hatia ya jinai itabainika, Mamlaka itatoa mapendekezo, ikiwa ni pamoja na lakini sio tu kufunguliwa mashtaka," aliongeza.

Whitney alikuwa mwanafunzi wa kidato cha nne katika Shule ya Sekondari ya Nakuru Central.

Makori alisema uchunguzi wa mauaji yake utakuwa huru, usio na upendeleo na wa haki.

View Comments