In Summary

•Bw Wainaina alidai majibu kutoka kwa shule  kwani binti yake hakuwa na matatizo ya kiafya na hajawahi kuitwa na shule kuhusiana na matatizo yoyote ya kiafya pia.

•Familia hiyo sasa inasema haitasimamia hapo bali itafikia undani wa suala hili huku wakisubiri uchunguzi wa maiti 

Rip
Image: HISANI

Familia moja katika eneo la Njoro, kaunti ya Nakuru inaomboleza kwa uchungu baada ya binti yao wa kidato cha kwanza kufariki katika hali isiyoeleweka katika shule ya wasichana ya Njoro siku ya Alhamisi.

Baba ya marehemu, Bw. Peter Wainaina ambaye bado yuko katika hali ya mshtuko mkubwa baada ya kupokea habari hizo za kuhuzunisha, alidai majibu kutoka kwa shule  kwani binti yake hakuwa na matatizo ya kiafya na hajawahi kuitwa na shule kuhusiana na matatizo yoyote ya kiafya pia.

Alisema kuwa alipokea tu simu kutoka shuleni akielekezwa aende katika hospitali ya kaunti ndogo ya Njoro ambako bintiye, Whitney Njoki alikuwa amepelekwa.

Baada ya kuwasili, mkuu wa shule alimuelekeza kwa madaktari ambao walimpasha habari hiyo ya kusikitisha.

“Kwa muda, nilibaki kimya na kujawa na hasira nikihoji kwa nini wasimamizi wa shule hawakuchukua hatua za haraka kuokoa maisha ya binti yangu,” alisema Wainaina.

Baba huyo aliyevunjika moyo ulivunjika hakuweza kushikilia machozi yake wakati akisimulia kilichotokea, alisema  alikuwa akimtarajia binti yake wiki ijayo kwa mapumziko ya katikati ya muhula ila bahati mbaya kutokea.

"Binti yangu alijiunga na shule mnamo Februari 7 na tulikuwa na hamu arudi nyumbani na kutwambia ilivyokuwa katika shule ya upili," alibainisha Wainaina.

Familia hiyo sasa inasema haitasimamia hapo bali itafikia undani wa suala hili huku wakisubiri uchunguzi wa maiti ulioratibiwa kubaini sababu ya kifo. Mwili wa Njoki umelazwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha Chuo Kikuu cha Egerton.

Uongozi wa shule haukuweza kupatikana kuzungumzia suala hilo.

View Comments