In Summary

•"Ruto akiondoka, basi nini? Ruto anaweza kuondoka halafu Gachagua anachukua na kuendelea kutekeleza sera mbaya.

•Mivutano ilifikia kilele chake wakati kiongozi wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka alitimuliwa ghafla wakati alipokuwa akitoa maazimio ya kupinga kujiunga na serikali

Viongozi wa upinzani wa Azinio Coalition
Image: HISANI

Kiongozi wa upinzani na mgombea wa Uenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika (AUC), Raila Odinga, ameonyesha msimamo imara, akipuuzilia mbali wito wa Rais William Ruto kujiuzulu, licha ya shinikizo kuzidi na mvurugano wa ndani kwenye  mrengo wa upinzani.

Akizungumza na wanachama wa Kundi kutoka Bunge la Orange Democratic Movement (ODM), Odinga alisisitiza kuwa kumuondoa Ruto kutoka madarakani kutapelekea Naibu Rais Rigathi Gachagua kuchukua madaraka na kuendeleza sera mbaya.

"Ruto akiondoka, basi nini? Ruto anaweza kuondoka alafu Gachagua anachukua na kuendelea kutekeleza sera mbaya.

Ruto pia anaweza kusema 'Nimechoka, acheni majenerali wachukue madaraka'  halafu nchi inaanza kupitia yale ambayo Misri ilipitia baada ya Tahrir Square.

'Ruto lazima aondoke' haiwezi kuwa suluhu," Odinga alisema.

Aidha, "Ni wakati wa mgogoro kama huu ambapo nchi inahitaji kuzungumza. Hatufanyi hivi kumwokoa Ruto. Tunafanya hivi kuokoa Kenya.

Majenerali hawana vitoa machozi wala mizinga ya maji ila wana risasi."

Msimamo thabiti wa Odinga unaashiria pengo kubwa ndani ya upinzani, hasa ndani ya mrengo wa Azimio la Umoja One Kenya .

Mivutano ilifikia kilele chake wakati wa mkutano wa hivi majuzi wa Kundi la Bunge la ODM, ambapo kiongozi wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka, ambaye ni mmoja wa viongozi wa Azimio, alitimuliwa ghafla wakati alipokuwa akitoa maazimio ya kupinga kujiunga na serikali.

Hotuba ya Musyoka ilisambaratishwa na vijana wenye vurugu muda mfupi baada ya kuanza kusoma maazimio, huku Odinga tayari akiwa amejiondoa kwa ajili ya majukumu mengine.

La kushangaza zaidi, viongozi wakuu wa ODM, akiwemo aliyekuwa magavana Hassan Joho (Mombasa) na Wycliffe Oparanya (Kakamega), pamoja na Katibu Mkuu Edwin Sifuna na Mkurugenzi wa Masuala ya Siasa Junet Mohamed, hawakumfuata Musyoka kwenye mkutano na waandishi wa habari, ishara ya migawanyiko zaidi ndani ya safu za upinzani.

Aliyekuwa Gavana wa zamani wa Mombasa na Naibu Mkuu wa ODM Hassan Joho alitoa usaidizi mkubwa kwa kushirikiana na Rais Ruto.

"Tunapaswa kutambua ni nini kinachofanya kazi kwetu kama ODM.

Sisi ni chama kikubwa zaidi ndani ya Azimio na hatuwezi kubughudhiwa," Joho alitangaza, akimlaumu Musyoka kwa kujaribu kumchafua Odinga kama msaliti wakati huo huo akishirikiana na Gachagua.

Mgawanyiko ndani ya Azimio ulitokea baada ya Rais William Ruto kutangaza jukwaa la mazungumzo ya siku sita ya kisekta mbalimbali itakayoanza Jumatatu, Julai 15.

Akizungumza Jumanne, Julai 9 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Kenyatta (KICC) huko Nairobi, Ruto alisema kwamba jukwaa litahusisha wawakilishi kutoka vyama vya siasa, vikundi vya kidini, jamii za kiraia, waajiri na vijana kujadili masuala muhimu ya kitaifa.

"Kwa lengo la kuhakikisha tunafuata bajeti yetu, washiriki wote watagharamia gharama zao za kuhudhuria. Uamuzi huu unafuatia mashauriano yaliyofanyika leo asubuhi," Ruto alitangaza.

Aliongeza kuwa wadau walihitajika kuwasilisha wawakilishi wao ifikapo Ijumaa ya wiki hiyo.

View Comments