ighalo

Odion Ighalo anasema alitamani sana kujiunga na Manchester United kiasi cha kukubali kupunguziwa mshahara ili kufanikisha mkataba na hakulala siku ambayo mkataba uliafikiwa. Mchezaji huyo wa miaka 30 raia wa Nigeria amejiunga na United kwa mkopo kutoka Shaghai Shenhua hadi mwisho wa msimu huu.

Mchezaji huyo wa zamani wa Watford anasema mamake alitokwa na machozi aliposikia habari hio. Ighalo anasema amekuwa shabiki wa United tangu utotoni na anafurahi kufanikisha ndoto yake ya kuichezea klabu hio.

Mkusanyiko wa habari za spoti;

Vilabu vya ligi ya Premier vinatarajiwa kufanyia mabadiliko dirisha la uhamisho la majira ya joto na kuiainisha na ya maeneo mengine Uropa. Kwa misimu miwili iliyopita dirisha la Uingereza lilifungwa siku moja kabla ya ligi hio kuanza. Hata hivyo makataa ya vilabu vingi vya Uropa yanakamilika mwishoni mwa mwezi Agosti na kupelekea vilabu hivyo kusema si sawa.

Suala hili litajadiliwa na maafisa wakuu wa vilabu vyote 20 vya ligi ya Primia watakapokutana hii leo.

Kocha wa Chelsea Frank Lampard yuko kwenye malumbano na klabu hiyo kuhusu kumuuza mlinda mlango wa uhispania Kepa Arrizabalaga mwenye umri wa miaka 25. Lampard anataka mlinda mlango wa Burnley na Uingereza Nick Pope wa miaka 27 kuchukua nafasi ya Arrizabalaga. Kwingineko Kiungo wa Uingereza James Maddison, mwenye umri wa miaka 23, yuko mbioni kukubali ofa mpya na Leicester.

Afisa mkuu mtendaji wa KPL Jack Oguda anasema bila ya ushahidi wa kutosha hawawezi kuchunguza visa vya kupanga mechi. Matamshi yake yanajiri siku mbili baada ya wachezaji watatu wa Kakamega Homeboyz walipigwa marufuku ya shughuli zote za soka na FIFA kwa kushawishi mechi kinyume cha sheria. Oguda anasema wanaweza tu kuchunguza visa hivyo, ikiwa watapokea ushahidi wa kutosha kutoka kwa mtu yoyote kwenye vilabu vya humu nchini.

Ulinzi Stars wamepata pigo kubwa katika juhudi zao za kushinda taji la KPL kwani kiungo Oscar Wamalwa atakaa nje kwa muda wa msimu uliosalia. Mshambulizi huyo wa Harambee Stars hatacheza hadi msimu ujao baada ya kupata jeraha la bega katika mechi yao dhidi ya AFC Leopards wikendi uliyopita. Wamalwa, mshindi wa Golden Boot, katika tuzo za Cecafa Senior Challenge mwaka uliopita, aligongana na mlinzi Collins Shivachi katika dakika za mwisho za mechi hio, na atarajiwa kufanyiwa upasuaji.

Nahodha wa timu ya raga ya Kenya Sevens Andrew Amonde anatarajiwa kufanyiwa uchunguzi wa goti wiki hii, ili kutathmini jeraha lake kabla ya timu hio kuregelea mazoezi wiki ijayo. Amonde alipata jeraha hilo wikendi iliyopita katika michuano ya Sydney Sevens ambapo Kenya ilimaliza katika nafasi ya 16. Kocha Paul Feeney anatumai kwamba jeraha la Amonde halitamweka nje ya misururu ya Los Angeles na Vancouver Sevens.

View Comments