In Summary

•Mustakabali wa mabingwa wa Ulaya Chelsea haujulikani baada ya vikwazo kuwekewa mmiliki wa Urusi Roman Abramovich siku ya Alhamisi.

Mmiliki wa Chelsea Roman Abramovich
Image: BBC

Mustakabali wa mabingwa wa Ulaya Chelsea haujulikani baada ya vikwazo kuwekewa mmiliki wa Urusi Roman Abramovich siku ya Alhamisi.

Bilionea huyo amekuwa akiiongoza klabu hiyo tangu 2003 lakini majaribio yake ya kutaka kuiuza klabu hiyo yalisitishwa na serikali ya Uingereza, ambayo imezuia mali yake.

Ina maana gani kwa mashabiki, wachezaji na wafanyakazi wa Chelsea? BBC Sport inaeleza jinsi hali hiyo itaathiri wale wanaohusishwa na klabu hiyo.

Ni nini hasa kilitokea Alhamisi?

Abramovich aliwekewa vikwazo na serikali ya Uingereza kama sehemu ya majibu yake kwa uvamizi wa Urusi dhidi ya Ukraine.

Serikali inaamini kuwa bilionea huyo amekuwa na "uhusiano wa karibu kwa miongo kadhaa" na rais wa Urusi Vladimir Putin, viungo ambavyo Abramovich amekuwa akikanusha.

Kama mali yake yote, Chelsea ingefungiwa lakini leseni maalum iliyotolewa na serikali inaruhusu klabu hiyo ya Stamford Bridge kuendelea kufanya kazi.

Je, Chelsea wanaweza kuendelea kucheza mechi?

Ndiyo.

Leseni maalum iliyotolewa na serikali inaruhusu timu za wanaume na wanawake kutimiza ratiba zao kwa msimu huu wote kama kawaida.

Vijana wa Chelsea walishinda Norwich katika Ligi ya Premia Alhamisi usiku huku timu ya wanawake ya Chelsea ikicheza dhidi ya West Ham kwenye Ligi Kuu ya Wanawake kwa wakati mmoja.

Ina maana gani kwa mashabiki wanaoenda mechi?

Wamiliki wa tikiti za msimu bado wataweza kuhudhuria michezo huko Stamford Bridge kama kawaida, huku tikiti za mechi zinazouzwa kabla ya Machi 10 zikiuzwa .

Image: REUTERS

Lakini zaidi ya hapo, mashabiki hawawezi kununua tikiti zozote mpya kutazama Chelsea.

Tikiti zilipaswa kuuzwa kwa mechi ya robo fainali ya Kombe la FA huko Middlesbrough mnamo Machi 19 lakini chapisho kwenye wavuti rasmi wa kilabu mnamo Alhamisi lilithibitisha kwamba haingefanyika tena kama ilivyopangwa.

Klabu hiyo pia haiwezi kuuza bidhaa yoyote, huku duka la kilabu la Stamford Bridge likifungwa Alhamisi asubuhi.

Je, Chelsea wanaweza kuuza tikiti za msimu ujao?

Mwandishi mwandamizi wa habari za michezo wa BBC Laura Scott:

Leseni yote inasema ni kwamba mtu yeyote ambaye alinunua tikiti za msimu kabla ya leo, na kufanya malipo kwa awamu za kawaida, anaweza "kuendelea kufanya malipo hayo".

Hakuna kutajwa kwa misimu ijayo.

Je, Chelsea inaweza kuendelea kulipa mishahara ya wafanyakazi ndani ya muda mfupi na wa kati?

Leseni maalum ya serikali inaruhusu Chelsea kulipa mishahara ya wafanyikazi wote, pamoja na wachezaji na makocha.

Leseni ipo hadi Mei 31, kwa hivyo inashughulikia Blues kwa msimu uliosalia na Hazina ina haki ya kuibadilisha, kubatilisha au kuisitisha wakati wowote.

Je, vikwazo hivi vinamaanisha hawawezi kuhamisha wachezaji ndani au nje?

Mustakabali wa Antonio Rudiger katika klabu ya Chelsea haujulikani kwa kandarasi yake inaisha msimu wa joto
Image: GETTY IMAGES

Wakati vikwazo hivyo vikiendelea, Chelsea iko chini ya marufuku ya uhamisho na haiwezi kununua wala kuuza wachezaji.

Pia hawawezi kujadili mikataba mipya kwa wachezaji wanaomiliki kwa sasa, kwa hivyo inaacha mustakabali usio na uhakika kwa wale ambao mikataba yao ya sasa inaisha msimu wa joto.

Hiyo inawahusu Antonio Rudiger, Cesar Azpilicueta, na Andreas Christensen, ingawa wawili hao wa mwisho wamehusishwa na kuhamia Barcelona.

Rudiger aliaminika kukaribia mkataba mpya lakini hatua ya sasa inamwacha beki huyo katika hali ya kutatanisha.

Vipi kuhusu mustakabali wa makocha wakuu wa wanaume na wanawake wa Chelsea?

Simon Stone wa BBC Sport:

Ni hali sawa kwa Thomas Tuchel na Emma Hayes - hakuna mtu ana wazo lolote jinsi hii itawaathiri bado.

Wana mikataba, hakuna anayesema hawatalipwa. Hata hivyo huu ni wakati wa mabadiliko makubwa. Je, inaifanya klabu kuwa katika hatari zaidi ya kupata meneja yeyote kutoka kwa timu pinzani? Mambo huenda yakabadilika kwa kiasi kikubwa katika klabu.

Tuchel bado hajatoa maoni yake kuhusu kilichofanyika Alhamisi, ingawa bila shaka ataulizwa kuhusu hilo baada ya mechi ya Chelsea huko Norwich baadaye siku hiyo hiyo, na kwa hivyo hali yake inaweza kuwa wazi zaidi wakati huo.

Thomas Tuchel na Emma Hayes wanafundisha timu za wanaume na wanawake mtawalia
Image: GETTY IMAGES

Hayes, ambaye amekuwa katika klabu hiyo kwa muongo mmoja, alitia saini kandarasi ya muda mrefu mwezi Julai na alikuwa na jicho la kutafuta taji la kwanza la Ligi ya Mabingwa akiwa na Chelsea.

Anaungwa mkono sana ndani ya klabu na amepata heshima kutoka kwa wale walio juu, akiwa ameshinda mataji 10 makubwa wakati wa uongozi wake.

Hayes pia alikuwa miongoni mwa orodha ya kipekee ya wadhamini ambao Abramovich alijaribu kuwapa 'usimamizi' wa Chelsea mwishoni mwa mwezi uliopita. Dhamira yake kwa klabu haijawahi kutiliwa shaka hivyo mashabiki bila shaka watakuwa wakifuatilia hali hiyo kwa tahadhari.

Je, Chelsea bado inaweza kuuzwa?

Alistair Magowan wa BBC Sport:

Chelsea ilitangazwa kuuzwa tarehe 2 Machi na inafahamika kuwa kuna watu wengi wanaovutiwa, licha ya Abramovich kuwekewa vikwazo.

Serikali ya Uingereza iko tayari kuzingatia nyongeza zaidi kwa leseni maalum ili kuruhusu mauzo kuendelea.

Wale wanaofanya kazi katika mpango huo kwa niaba ya Abramovich waliambiwa kila mara kuwa mapato kutoka kwa mauzo yangeenda kwa hazina ya vita kwa wahasiriwa wa vita nchini Ukraine.

Hili liliwekwa wazi wakati Abramovich alipotangaza kuiuza klabu hiyo wiki jana. Inafahamika kuwa mkopo wa £1.5bn kutoka kwa Abramovich hautakatwa kwenye bei hiyo.

Abramovich alikuwa ameiagiza kampuni ya uwekezaji ya Marekani ya Raine Group kutafuta pauni bilioni 3 kwa klabu hiyo, lakini wataalam wa masuala ya fedha wanaamini kwamba bei ambayo tayari imepanda inaweza kushuka zaidi kutokana na kutokuwa na uhakika kwa Chelsea.

Jinsi klabu inaweza kuuzwa haraka pindi mnunuzi atakapopatikana inategemea na serikali kupokea hakikisho kwamba mapato hayataenda kwa Abramovich, lakini kupata uhakikisho huo kunaweza kuchukua muda.

Vipi kuhusu ushiriki wa Chelsea katika mashindano ya Ulaya?

 

Kikosi cha wanaume cha Chelsea kilishinda Ligi ya Mabingwa msimu uliopita huku timu ya wanawake ikishika nafasi ya pili
Image: GETTY IMAGES

Mwandishi mwandamizi wa habari za michezo wa BBC Laura Scott:

Yote ambayo tumekuwa nayo kutoka Uefa katika hatua hii ni kwamba 'inatafuta ufafanuzi zaidi juu ya suala hilo' kabla ya kutoa maoni zaidi.

Kile ambacho Uefa inakisiwa kukianzisha ni kile kitakachotokea iwapo Chelsea itafuzu robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, na haiwezi kuuza tikiti zozote.

Ikiwa Chelsea itatinga nusu fainali ya Kombe la FA, je, sehemu yao ya uwanja itakuwa tupu?

Kikosi cha wanaume cha Chelsea kiko ugenini dhidi ya Middlesbrough inayoshiriki Championship katika robo-fainali tarehe 19 Machi (17:15 GMT) ambayo itaonyeshwa moja kwa moja kwenye BBC One.

Iwapo watashinda hilo basi watacheza huko Wembley katika nusu-fainali wikendi 16-17 Aprili.

Haijulikani kwa wakati huu jinsi vikwazo hivyo vitaathiri mauzo ya tikiti za Kombe la FA ikiwa watasonga mbele hadi Wembley.

Je, Chelsea wanaweza kumudu usafiri wa ugenini, kwa kuzingatia bajeti ya serikali?

Mwandishi mwandamizi wa habari za michezo wa BBC Laura Scott:

Serikali imeweka kikomo cha pauni 20,000 kwa kila timu kwa mechi kwa ajili ya kusafiri kwenda na kurudi kwenye mechi.

BBC Sport inaelewa kuwa klabu hiyo inachukulia kama kitita cha pauni 20,000 kuwa chini sana kuiruhusu kufanya kazi kama kawaida, na hili ni suala la dharura kutokana na wiki ijayo kuwa timu ya wanaume itasafiri hadi Lille katika Ligi ya Mabingwa.

Je, wadhamini wa Chelsea wana thamani gani na wamepokeaje?

Saa chache baada ya kutangazwa kuwa Abramovich amewekewa vikwazo na serikali ya Uingereza, wadhamini wakuu wa jezi za Chelsea walisitisha mkataba wao wa pauni milioni 40 kwa mwaka na klabu hiyo.

Mtoa huduma wa mtandao wa simu Three amekuwa mshirika rasmi wa Chelsea tangu 2020.

Haijulikani iwapo mkataba wowote wa udhamini wa Chelsea uko hatarini kwa wakati huu.

Mnamo mwaka wa 2016, kilabu cha London kilisaini mkataba mpya wa jezi na kampuni kubwa za mavazi ya michezo ya Amerika Nike. Wakati huo iliripotiwa kuwa na thamani ya £60m kwa msimu kwa miaka 15 iliyofuata, lakini klabu haikuthibitisha takwimu zozote za fedha.

Mnamo Mei 2021, Chelsea ilitaja jukwaa la utafutaji hoteli duniani trivago kama mshirika rasmi wa mafunzo ya klabu katika ushirikiano wa miaka mingi.

Chelsea pia ina idadi ya washirika wengine rasmi.

Je, Chelsea inaweza kuwekwa chini ya mrasimu?

Iwapo Chelsea hawataweza kulipa bili zao wanaweza kuingia kwenye urasimu na kukatwa pointi tisa.

Mwanahabari wa masuala ya fedha Kieran Maguire:

Kwa muda mfupi, ni kwa kiasi kikubwa hali ya biashara itaendelea kama kawaida. Chelsea wataweza kulipa mishahara inayotakiwa mwishoni mwa Machi na watakuwa na nyongeza nyingine.

Malipo ya mshahara wa Chelsea ni takriban £28m kwa mwezi. Hatujui wana pesa ngapi benki. Akaunti za hivi majuzi zaidi tulizo nazo ni za Juni 2021 wakati benki ilikuwa £16m. Abramovich amekuwa akiiingizia Chelsea pesa mara kwa mara katika miaka ya hivi karibuni na huenda hilo halitaweza kuendelea.

Wasiwasi unaweza kuwa kile kinachotokea ikiwa akiba ya pesa ya Chelsea haitoshi kulipa bili yao ya mishahara - lakini huenda serikali na Ligi ya Premia, ambao wamekuwa wakilifanyia kazi hili, watakuwa wakiliangalia ili kujaribu kupunguza usumbufu katika ngazi ya klabu.

View Comments