In Summary

• “Kuna Messi mmoja tu kama ambavyo kila mtu aliona katika mashindano ya kombe la dunia" - Ten Hag alisema.

• Alisema kuwa wachezaji wengine waendelee tu kujituma kuwakilisha timu zao lakini suala la GOAT liachiwe Messi.

Ten Hag amchokoza Ronaldo kuhusu suala la GOAT
Image: Twitter

Kwa karibia miongo miwili sasa, kumekuwa na mjadala mkali kuhusu ni mchezaji yupi katika kizazi hiki cha sasa kati ya Ronaldo Christiano na Lionel Messi anafaa kuvikwa kiremba cha ubingwa kama fundi wa soka – GOAT.

Gumzo hilo kila mtu hulichanganua kwa njia yake, na sababu zake za kutetea chaguo lake la GOAT baina ya wachezaji hao wawili ambao wamekuwa katika viwango vya juu kwenye ulingo wa soka kwa zaidi ya miaka 16 sasa.

Wikendi iliyopita, kocha mkuu wa Manchester United Eric Ten Hag alikuwa kikaangoni kutoa tamko lake kuhusu ni nani anayefaa kuvishwa taji la GOAT katika malimwengu ya soka baina ya Messi wa Argentina na Ronaldo wa Ureno.

Ikumbukwe pia kuwa kocha huyo walichafuana vikali na mchezaji Ronaldo mwishoni mwa mwaka jana baada ya kutofautiana kwa maneno.

Ten Hag alikuwa anamkalisha Ronaldo kwenye benchi licha ya mchezaji huyo kuwa kweney fomu nzuri, jambo ambalo lilichangia pakubwa kukosana kwao na Ronaldo akafanya mahojiano akiweka wazi kuwa hawezi kuwa na heshima kwa Ten Hag kwa vile kocha huyo mwanzo alimkosea heshima.

Sasa Ten Hag kipindi cha kujibu swali hilo, alimtupia bomu la kichwani Ronaldo huku akisema kuwa yeye hajawahi msikia wala kumuona na mtu ambaye anatambua katika soka ni Messi pekee.

“Kuna Messi mmoja tu kama ambavyo kila mtu aliona katika mshindano ya kombe la dunia. Lakini hao wengine ni sharti tu wajitume kufanyia timu zao kazi,” Ten Hag alijibu huku maneno yake kumtambua Messi pekee yakitajwa kama mkwara kwa Ronaldo.

Kauli ya Ten Hag itazua maswali kuhusu mtazamo wa Ronaldo katika kipindi cha miezi mitano chini yake. Nyota huyo wa Ureno alikosolewa kila mara na baadhi ya mashabiki kwa kuwa mbinafsi hasa baada ya kutoka nje ya uwanja wakati wa mchezo wa Ligi Kuu ya England kwenye Uwanja wa Old Trafford.

Ronaldo amehamia Al-Nassr akionekana kumaliza maisha yake ya muda mrefu na yenye mafanikio makubwa Ulaya.

 

View Comments