In Summary

•Uingereza na Uholanzi ziliwashinda wapinzani wao na kujipatia nafasi ya kusalia katika kinyang'anyiro hicho.

•Uhispania sasa itamenyana na Ufaransa katika nusu fainali mnamo Julai 9 huku Uholanzi ikipimana nguvu na Uingereza Julai 10.

Uingereza ilipiga Uswizi na kufuzu kwa nusu fainali
Image: HISANI

Mashindano ya Euro 2024 yameingia rasmi katika  hatua ya nusu fainali.

Hii ni baada ya mechi mbili za mwisho za robo fainali kuchezwa siku ya Jumamosi usiku huku Uingereza na Uholanzi zikiwashinda wapinzani wao na kujipatia nafasi ya kusalia katika kinyang'anyiro hicho.

Timu hizo mbili zilipambana kutoka nyuma na kutwaa ushindi baada ya wapinzani wao kupata nafasi ya kufunga bao la kwanza.

Katika mechi ya kwanza iliyochezwa mwendo wa saa moja Jumamosi usiku, wapinzani wa England wa mechi hiyo, Uswizi walipata bao la kwanza dakika ya 75 kupitia kwa mshambuliaji mahiri wa Monaco, Breel Embolo.

Dakika tano tu baadaye, mshambuliaji Bukayo Saka alipokea pasi nzuri kutoka kwa mchezaji mwenzake katika Arsenal Declan Rice kufunga bao la kusawazisha la England.

Mchuano huo ulimalizika kwa sare ya 1-1, huku dakika 30 za nyongeza pia zikimalizika kwa sare ya bila kufungana, ikimaanisha kuwa pambano hilo lilitakiwa kuamuliwa kwa njia ya penalti.

Ilikuwa ni wakati wa mikwaju ya penalti ambapo England walifunga nafasi zao zote huku beki wa Man City Manuel Akanji akishindwa kufunga shuti lake kwa Uswisi.

Uholanzi pia walipambana kutoka nyuma kwenye mechi yao dhidi ya Uturuki baada ya wapinzani wao kufunga bao la kwanza dakika ya 35.

Kipindi cha pili, Uholanzi walirejea uwanjani wakiwa na nguvu mpya iliyowasaidia kufunga mabao mawili katika dakika ya 70 na 76. Bao la kwanza lilifungwa na beki Stefan de Vrij huku la pili likifungwa na Mert Muldur.

Uhispania sasa itamenyana na Ufaransa katika mechi ya nusu fainali ya kwanza itakayochezwa Julai 9 huku Uholanzi ikipimana nguvu na Uingereza Julai 10.

 Fainali za shindano hilo zitachezwa Julai 14 mjini Berlin.

View Comments