In Summary

•Smith Rowe aliondoka Arsenal Agosti 2 baada ya kuwa katika klabu hiyo yenye maskani yake London kwa takriban miaka minane.

•Arteta alibainisha kuwa kiungo huyo alikuwa sehemu muhimu ya klabu na akakiri  alishindwa kumsaidia kufikia uwezo wake.

Kocha Mikel Arteta amekiri kuhuzunishwa na kuondoka kwa Smith Rowe
Image: HISANI

Meneja wa klabu ya Arsenal Mikel Arteta amevunja ukimya kuhusu uchungu ambao alihisi baada ya kumpoteza kiungo Emile Smith Rowe mapema mwezi huu.

Smith Rowe aliwaaga Wanabunduki na kujiunga na Fulham mnamo Agosti 2 baada ya kuwa katika klabu hiyo yenye maskani yake London kwa takriban miaka minane.

Akiongea na wanahabari kabla ya mechi ya Aston Villa dhidi ya Arsenal siku ya Jumamosi, kocha Mikel alibainisha kuwa kiungo huyo mwenye umri wa miaka 24 alikuwa sehemu muhimu sana ya klabu na akakiri kwamba alishindwa kumsaidia kufikia uwezo wake.

"Yeye (Smith Rowe) alikuja kwenye timu wakati ulikuwa mgumu. Alikuwa mchezaji aliyewafanya mashabiki wetu na timu kuingiana, sijui jinsi ya kuielezea. Nina hisia kwamba sikupata bora kutoka kwake. Kwa upande wangu, ilikuwa ya kusikitisha sana,” Mikel Arteta aliwaambia waandishi wa habari.

Kocha huyo mwenye umri wa miaka 42 alikiri wazi kwamba haikuwa wakati rahisi kwake kuona Smith Rowe akiondoka katika klabu hiyo.

"Nilihuzunika wakati Smith-Rowe alipotuacha. Nilipokuwa na mazungumzo na Emile, nilihisi sana," alisema.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 24 alijiunga na Fulham kwa mkataba unaoripotiwa kuwa wa thamani ya £27m pamoja na nyongeza za £7m.

Arsenal walikuwa wamemkabidhi Smith Rowe jezi namba 10 baada ya kusaini mkataba mpya wa miaka mitano na klabu hiyo mnamo 2021.

Alicheza kwa mara ya kwanza kwenye kikosi cha kwanza cha Arsenal mwaka wa 2018, baada ya kuhitimu kutoka kwa akademia ya klabu hiyo

View Comments