In Summary

•Aliyekuwa waziri wa Mafuta na Madini John Munyes alikubali kushindwa katika kinyang’anyiro cha ugavana Turkana.

•Aliyekuwa Waziri wa Nishati na Petroli Charles Keter pia alikuwa amejiuzulu kazi yake na kujiunga na siasa.

Aliyekuwa waziri John Munyes
Image: MAKTABA

Mawaziri watatu waliojiuzulu kutoka serikalini ili kujitosa kwenye siasa wameshindwa.

Watatu hao walijiuzulu mnamo Februari 2022 kwa lengo la kunyakua nyadhifa za kuchaguliwa. Wengi wao walikuwa wakitafuta nyadhifa za ugavana.

Alhamisi, aliyekuwa waziri wa Mafuta na Madini John Munyes alikubali kushindwa katika kinyang’anyiro cha ugavana Turkana na kumpongeza mgombea wa ODM Jeremiah Lomurkai.

Munyes (Jubilee), Lomurkai (ODM) na John Lodepe wa UDA walikuwa wakipambana kumrithi gavana anayeondoka Josphat Nanok.

Alimtakia gavana mteule kila la heri na kumpa changamoto kutoa uongozi ufaao kwa watu wa kaunti ya Turkana.

"Nilipigana, uchaguzi ulikuwa wa amani sana Turkana licha ya changamoto chache za usafirishaji katika baadhi ya maeneo ya Turkana," alisema wakati akiwahutubia wanahabari huko Lodwar.

Aliyekuwa Waziri wa Nishati na Petroli Charles Keter pia alikuwa amejiuzulu kazi yake na kujiunga na siasa. Alikuwa akitafuta kiti cha ugavana kaunti ya Kericho.

Keter, hata hivyo, alishindwa katika mchujo wa chama cha United Democratic Alliance (UDA) uliofanyika Aprili 2022 na akakubali kushindwa na Erick Mutai.

Keter alikuwa amepata kura 60,342 pekee dhidi ya Mutai ambaye alikuwa na kura 126,038. Aliamua kutoendelea kukifuata kiti hicho.

Adan Mohammed, ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki katika utawala wa Rais Uhuru Kenyatta pia alikubali kushindwa katika kinyang'anyiro cha ugavana Mandera.

Alikubali kushindwa hata kabla ya maafisa wa IEBC kutangaza matokeo.

View Comments