In Summary

•Jungle alisema kuwa tayari ameiandikia barua tume ya uchaguzi na mipaka nchini (IEBC) na ameambatanisha ushahidi wa ukora huo.

Mwaniaji wa kiti cha ugavana wa Kiambu Wainaina jungle akihutubia wanahabari.Alisema kuwa alishinda kinyang'anyiro hicho lakini ushindi wake ukaibwa.Anadai kura zihesabiwe upya.
Image: AMOS NJAU

Mgombea ugavana wa Kiambu kwa tiketi ya kujitegemea Wainaina Jungle amesema atapinga ushindi wa mgombea wa UDA Kimani Wamatangi mahakamani.

Akizungumza siku ya Jumamosi, Jungle alisema kuwa zoezi hilo halikufanywa kwa njia ya uwazi.

Alitoa mfano kuwa baadhi ya mawakala wake walitupwa nje ya vituo vya kujumlisha kura.

Jungle alisema kuwa tayari ameiandikia barua tume ya uchaguzi na mipaka nchini (IEBC) na ameambatanisha ushahidi wa ukora huo.

"Ningependa kuiomba IEBC kutomtangaza Wamatangi kama mshindi kwani zoezi hilo lilikuwa na dosari nyingi," Jungle alisema.

Hapo awali, gavana wa Kiambu James Nyoro alikuwa amesema kuwa timu ya Jubilee iliyoko Kiambu itaenda mahakamani kama timu kuomba zoezi hilo lirudiwe.

"Tunajua kilichotokea na hatutaruhusu Wamatangi kutangazwa kuwa mshindi," Nyoro alisema.

Mgombea ubunge wa Thika David Ngari alisema kuwa hawataruhusu IEBC kutoa cheti kwa mtu ambaye hakushinda.

"Hatutakubali matokeo na tunaelekea mahakamani," alisema.

View Comments