In Summary

• "Raila Odinga hana budi kuchukua hatua madhubuti kukomesha uvujaji huu wa watu kuingia mrengo ule." - Kipkorir

Wakili Donald Kipkorir na rais Uhuru Kenyatta
Image: State House Kenya (Facebook), Donald Kipkorir (Twitter)

Mwanasheria Donald Kipkorir sasa ametilia shaka jinsi rais mteule William Ruto anavyoendelea kuwashawishi wale waliochaguliwa kama wagombea huru ili kujiunga na muungano wa Kenya Kwanza.

Kipkorir anasema kwamba huenda mahakama ya upeo wa juu ikabatilisha uamuzi wa tume huru ya mipaka na uchauzi IEBC kumkabidhi Ruto cheti cha ushindi katika uchaguzi wa urais uliofanyika wiki jana.

Kutokana na wasiwasi wake huo, sasa anamtaka rais anayeondoka Uhuru Kenyatta kuingilia kati na kumsaidia kinara wa Azimio Raila Odinga kupata urai kwani kulingana na yeye Odinga alishinda kihalali ila akadhulumiwa.

Kipkorir alisema kwamba Ruto ameanza mchakato wa kutongoza vyama tanzu vilivyounda muungano wa Azimio na kuvishawishi kujiunga na muungano wa Kenya Kwanza na kwamba hili linanuiwa kudhoofisha Azimio.

Anasema Kenyatta anafaa kulivalia njuga suala hilo na pia Raila kuchukua mipango Madhubuti ya mapema kabla ili kuzuia mchakato huo wa wanasiasa kujiunga na mrengo wa Dkt. Ruto.

“Mahakama ya upeo wa Juu inaweza kubatilisha Matokeo ya Urais, uongozi wa UDA uko mbioni kubadilisha hali ya kisiasa kwa kununua Wabunge wote Wanaojitegemea na Vyama vya Azimio. Raila Odinga hana budi kuchukua hatua madhubuti kukomesha uvujaji huu wa watu kuingia mrengo ule. SASA. Uhuru Kenyatta lazima asaidie,” Kipkorir alisema kupitia ukurasa wake wa Twitter.

Mwanasheria huyo ambaye ni mkereketwa nguli wa sera za Azimio la Umoja alionekana kukerwa na hatua ya wagombea walioshinda haswa kama wagombea huru na kusema ni juzi tu wamechaguliwa na hata kabla ya kuingia ofisini tayari wameshaanza kujitenga kwa kujiunga na mirengo ya kisiasa.

Ikumbukwe tangu juzi Ruto alipoitisha mkutano na washindi katika uchaguzi kupitia vyama tanzu vya Kenya Kwanza, aliwapokea makumi ya wagombea huru waliochaguliwa na jana alikipokea chama cha UDM ambacho awali kilikuwa moja ya vyama vilivyounda muungano pinzani wa Azimio la Umoja One Kenya.

 

View Comments