Juliani azungumzia madai ya kuteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Burudani wa muungano wa Azimio

Muhtasari
  • Juliani azungumzia madai ya kuteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Burudani wa muungano wa Azimio
Msanii Juliani
Image: Instagram/JUliani

Baada ya uvumi na madai kuenea mitandaoni kuwa ameteuliwa kuwa mkurugenzi wa burudani katika muungano wa Azimio, msanii Juliani ametoa taarifa na kukana madai hayo.

Madai hayo yalienea sana mitandaoni siku ya Jumatatu.

Kupitia kwenye taarifa hiyo, msanii huyo alisema kwaba hamna mazungumzo ya rasmi ambayo ameungumza na muungano wowote wa kisiasa, wala hajaandikwa na muungano wowote.

“Nimefahamishwa kuwa kuna habari inayosambazwa mtandaoni kuhusu kuteuliwa kwangu kama Mkurugenzi wa Burudani katika Muungano wa Azimio - OKA.

"Ningependa kufafanua kuwa hii haijawasilishwa kwangu rasmi au vinginevyo. Kwa hivyo ningependa kuthibitisha kuwa sijaajiriwa au kuhusishwa na chama chochote cha kisiasa nchini Kenya au kwingineko,” ilisema sehemu ya taarifa ya rappa huyo.

Hata hivyo aliongeza kuwa yuko tayari kushirikiana na viongozi wowote ambao wangependa kupata uzoefu wake katika utetezi na mipango ya biashara ya kijamii.

Juliani aliorodhesha miradi ambayo amesimamia kama vile kutetea uwezeshaji wa vijana kupitia ushauri kupitia Dandora HipHop City (DHC), kuanzisha suluhisho za Benki ya Taka ambayo inatoa ajira kwa vijana katika vitongoji duni na pia kuwa mwanaharakati wa haki za kijamii.

"Haya yaliyo hapo juu hayanipi anasa ya kujitenga na masuala ya utawala, hasa katika mwaka wa uchaguzi. Niko tayari kuungana na washirika wenye nia moja ikiwa ni pamoja na vyama vya siasa ambavyo vina ilani na ajenda iliyo wazi inayolenga hasa mipango endelevu ya kuwawezesha vijana,” mwanamuziki huyo alibainisha.

Aliongeza kuwa ana shauku kubwa ya sababu kama vile uwezeshaji wa vijana, usawa wa kijinsia na unyanyasaji wa kijinsia (GBV) kukomesha mauaji ya kiholela, kukuza haki za kijamii na mabadiliko ya hali ya hewa.

“Ningependa kuwasihi Wakenya wenzangu kutumia hekima na kuwapigia kura viongozi ambao wataleta mabadiliko na kuepuka kuingia katika mtego wa kupofushwa na takrima. Pia ningependa kuwakatisha tamaa wanasiasa kutumia vijana wetu kujinufaisha wao wenyewe.

“Kwa mashabiki wangu na Wakenya wote nasema asante kwa upendo mlionionyesha. Ninashukuru na Mungu akubariki,” Juliani alimalizia.