Awinja afunguka jinsi mamake alivyohangaika kuwalea baada ya babake kuaga dunia

Awinja amesema kuwa nia yake kubwa ni kumpa mamake maisha mazuri.

Muhtasari

•Awinja amechukua fursa hiyo kumsherehekea mzazi huyo wake na kumtakia heri ya siku ya kuzaliwa.

•Alifichua kuwa mama yake alijihusisha na biashara mbalimbali katika juhudi za kujaribu kukidhi mahitaji ya familia.

Awinja na Mama yake
Image: INSTAGRAM// JACKY VIKE

Hivi leo, Disemba 15, mama ya muigizaji na mchekeshaji Jacky Vike almaarufu Awinja kutokana na kipindi cha Papa Shirandula kwenye Citizen TV anaadhimisha siku yake ya kuzaliwa.

"Siwezi kutulia ni siku ya kuadhimisha kuzaliwa kwa mama yangu! Mwamba wangu, kila kitu changu," alisema kupitia ukurasa wake wa Instagram.

Wakati huo huo, muigizaji huyo alisimulia jinsi mama yake alivyohangaika ili aweze kumlea yeye pamoja na ndugu zake. Hii ni baada ya baba yake mzazi kuaga dunia wakati yeye angali akiwa mtoto.

"Huyu mama alihangaika na sisi na mshahara ya Kanjo! Yenye ilikuwa inatoka baada ya miezi minne au zaidi, tuliishi," alisema.

Alifichua kuwa mama yake alijihusisha na biashara mbalimbali katika juhudi za kujaribu kukidhi mahitaji ya familia.

Miongoni mwa bidhaa ambazo mamake Awinja aliuza ni pamoja na miguu ya kuku, mboga, sigara na nyinginezo.

Kutokana na mahangaiko aliyopitia, Awinja amesema kuwa nia yake kubwa ni kumlipa mamake kwa kumpa maisha mazuri.

"Heri ya siku ya kuzaliwa Mamuu! Mrasta, Mariamu, Mkeree, Bibii. Naomba Mungu aendelee kukulinda kwa ajili yetu, tunakupenda,"

Mchekeshaji huyo aliambatanisha ujumbe huo wake na picha nzuri ya mama yake ambaye anaonekana katunzwa vizuri.

Aidha, alifichua kuwa Manispaa ya Nairobi ina deni ya mzazi huyo wake kutoka miaka kumi iliyopita.

"Alafu watu wa City Hall Mamangu bado anafuata pesa yake ya kustaafu kwa takriban miaka kumis sasa, mtu amwambie Sakaja," alisema.

Awinja aliwaomba wanamitandai kumsaidia kumsherehekea mama yake huku akiahidi kusoma jumbe zao kwake.