Richie Spice kutumbuiza Kisumu mnamo Mei 28, Nyong'o athibitisha

Tamasha hilo limefadhiliwa na Serikali ya Kaunti ya Kisumu na Ziva Empire.

Muhtasari

•Mwanamuziki huyo wa Reggea na Dancehall atakuwa na shoo ya moja kwa moja kwenye uwanja wa Mamboleo Show.

•Richie Spice alisema atakuwa akitumbuiza katika tamasha la Goods Vibes katika uwanja wa KICC mnamo Mei 27.

Mwimbaji Richie Spice
Image: HISANI

Mwanamuziki wa reggae kutoka Jamaica, Richell Bonner anayefahamika zaidi kama Richie Spice anatarajiwa kutumbuiza mjini Kisumu mnamo Mei 28, Gavana Anyang' Nyong'o amethibitisha.

Bango linalotangaza tukio hilo lililowekwa kwenye Twitter na kiongozi huyo wa kaunti linaonyesha kuwa msanii huyo wa reggea atakuwa na shoo ya moja kwa moja kwenye uwanja wa Mamboleo Show.

"Inakuja nyumbani! Jitayarishe kwa Mei 28 kwa shoo kubwa ya moja kwa moja ya Richie Spice katika Viwanja vya Mamboleo ASK," Nyong'o alisema.

Tamasha hilo limefadhiliwa na Serikali ya Kaunti ya Kisumu na Ziva Empire.

Richie Spice alithibitisha ziara yake nchini Kenya wiki tatu zilizopita kupitia Instagram akisema atakuwa akitumbuiza katika tamasha la Goods Vibes katika uwanja wa KICC mnamo Mei 27.

"Mei 27, Nairobi Kenya nitakuja upate tikiti yako sasa ubarikiwe!"

Msanii huyo maarufu wa reggea, mwanachama wa vuguvugu la Rastafari, ana makumi ya nyimbo kwa jina lake.

Miongoni mwa nyimbo zake maarufu ni pamoja na 'Earth a Run Red', 'Brown Skin', 'Grooving' My Girl', 'Marijuana' na 'King and Queen.'

Richie Spice anatoka katika familia ya muziki ambapo ndugu zake wawili; Spanner Banner na Pliers wa kundi maarufu la Chaka Demus na Pliers pia wamejipatia jina.

Ndugu zake wengine Glenroy Bonner na Jah Mikes pia wamejaribu katika muziki lakini si maarufu kama Spice, Banner na Pliers.

Hii haitakuwa mara ya kwanza kwa Spice kutumbuiza nchini Kenya.

Mnamo 2017, alitumbuiza wakati wa Tamasha la Dobba pamoja na nyota wenzake wa Jamaika Etana na Luciano.

Spice alirejea miaka miwili baadaye mwaka wa 2019 na akatumbuiza kwenye tamasha la 'Nobody Can Stop Reggae'.