Wazazi wenza wa Diamond, Zari na Tanasha Donna wakumbatia muungano mzuri wa watoto wao

Zari Hassan na Tanasha Donna wanaonekana kufurahia sana uhusiano mzuri baina ya watoto wao.

Muhtasari

•Zari Hassan alichapisha picha ya watoto hao watatu wakiwa pamoja na kueleza waziwazi upendo wake mkubwa kwao.

•Tanasha pia alishiriki picha hiyo na kueleza upendo wake kwa watoto hao kupitia ukurasa wa Instagram wa Naseeb Junior

Zari Hassan, Tiffah Dangote, Naseeb Jr, Prince Nillan, Tanasha Donna
Image: HISANI

Wapenzi wa zamani wa mwimbaji wa bongofleva Diamond Platnumz, Zari Hassan na Tanasha Donna wanaonekana kufurahia sana uhusiano mzuri baina ya watoto wao.

Katika siku chache zilizopita, watoto wa Zari na Diamond, Latiffah Dangote na Prince Nillan wamekuwa nchini Tanzania pamoja na baba yao na kaka yao wa kambo, Naseen Junior ambaye ni mtoto wa bosi huyo wa WCB na Tanasha Donna.

Siku ya Jumapili, mwanasosholaiti Zari Hassan ambaye kwa sasa ameolewa na mfanyabiashara wa Uganda, Shakib Cham Lutaaya alichapisha picha ya watoto hao watatu wakiwa pamoja na kueleza waziwazi upendo wake mkubwa kwao.

“Watoto wangu!” Zari aliandika kwenye picha hiyo aliyoiweka kwenye Instagram na kuambatanisha ujumbe wake na emoji ya moyo kuashiria upendo.

Mzazi mwenza wa mwisho wa Diamond, Tanasha Donna pia alishiriki picha hiyo na kueleza upendo wake kwa watoto hao kupitia ukurasa wa Instagram wa Naseeb Junior ambao anaudhibiti.

"Dada mkubwa & kaka mkubwa @princess_tiffah, @princenillan," yalisomeka maelezo kwenye picha iliyowekwa kwenye ukurasa wa Naseeb Junior.

Tiffah na Nillan ambao wanaishi Afrika Kusini na mama yao Zari Hassan waliwasili Tanzania na baba yao kuelekea mwishoni mwa wiki iliyopita na kuungana na kaka yao wa kambo Naseeb Junior ambaye amekuwa katika nchi hiyo jirani pamoja na mama yake Tanasha kwa wiki kadhaa zilizopita.

Siku ya Jumamosi,Diamond aliwasili akiwa ameandamana na watoto hao wake katika hafla ya Tuzo za Trace 2023 ambayo ilifanyika jijini Kigali, Rwanda.

Video na picha za hafla hiyo iliyopambwa na mastaa kutoka sehemu mbalimbali za bara Africa zilionyesha bosi huyo wa WCB akiwasili kwenye eneo la tukio huku akiwa ameshikana mikono na  wanawe, Latifah Dangote, Prince Nillan na Naseeb Jr.

Walioandamana nao pia ni mama yake, Mama Dangote na anayedaiwa kuwa mpenzi wake wa sasa, Bi Zuhura Othman almaarufu Zuchu.

Sita hao ambao wote walikuwa wamevalia mavazi ya kipekee waliingia ndani ya ukumbi wa tuzo huku wakiwa wameshikana mikono, pengine kuashiria wao ni familia. Zuchu na Tiffah walivaa nguo nyeupe huku Diamond na wanawe wawili wakiwa wamevalia nguo za kijani. Mama Dangote kwa upande  wake alivalia kitenge cha njano na nyeupe.