Itumbi amuomboleza kihisia marehemu Jahmby Koikai, afichua kumbukumbu zao nzuri

“Asante kwa kuniruhusu katika maisha yako. Safiri salama, Fyah Mumaah!" Itumbi aliomboleza.

Muhtasari

•Itumbi alizungumza kuhusu matukio mazuri ambayo alishiriki na marehemu mtangazaji huyo wa reggae aliyefariki Jumatatu usiku.

•Alikumbuka jinsi marehemu alivyojaribu kumfundisha jinsi ya kucheza densi za reggae, lakini hakuweza kuelewa.

amemuomboleza marehemu Jahmby Koikai.
Dennis Itumbi amemuomboleza marehemu Jahmby Koikai.
Image: HISANI

Mtaalamu wa masuala ya kidijitali Dennis Itumbi ameungana na maelfu ya Wakenya kuomboleza marehemu mtumbuizaji wa nyimbo za reggae Mary Njambi Koikai almaarufu Fyah Mummah Jahmby.

Katika taarifa iliyojaa hisia aliyoandika siku ya Jumatano asubuhi, Itumbi alizungumza kuhusu matukio mazuri ambayo alishiriki na marehemu mtangazaji huyo wa reggae aliyefariki Jumatatu usiku.

Alizungumzia jinsi marehemu Jahmby alivyopambana na ugonjwa wa endometriosis kwa zaidi ya miongo miwili na jinsi alivyojitahidi kuwasaidia wengine.

“Njambi Koikai. Nenda vizuri. Asante kwa kunisukuma hata wakati sikuelewa ulichokuwa unapigania, hadi nilipopata, sawa sio yote, lakini kwa kiasi kikubwa,” Itumbi alimuomboleza marehemu Jahmby Koikai kupitia kurasa zake za mitandao ya kijamii.

Aliongeza, "Miaka 21 ukipambana na maumivu. Upasuaji mara 10, 15, 20 na zaidi.. Kupigana kwa ajili ya wengine, hata wakati maumivu yako yalikuwa yanazidi kuwa makali zaidi. Unaondoka kama umeacha alama inayoonekana karibu na kila mtu aliyetazama safari yako."

Mtaalamu huyo wa mikakati wa kidijitali pia alikumbuka nyakati fulani za kusisimua alizokuwa nazo na Jahmby katika kipindi chote cha urafiki wao. Alikumbuka jinsi marehemu alivyojaribu kumfundisha jinsi ya kucheza densi za reggae, lakini hakuweza kuelewa.

"Lakini umenifanya nimjue Bob Marley na nukuu yake, "Huwezi kujua jinsi ulivyo na nguvu hadi kuwa na nguvu iwe chaguo lako pekee."  Kisha katika siku zako za mwisho, ulisukuma kupigana zaidi, kuelewa shida inayowakabili wasichana wengi - Thoracic Endometriosis- ulikufa ukinielimisha na kunisukuma," aliandika.

“Asante kwa kuniruhusu katika maisha yako. Safiri salama, Fyah Mumaah! Paulo alikuwa anaandika juu yenu, mmepigana vita vizuri, mmemaliza mwendo!” aliongeza.

Aliendelea kufariji familia na marafiki wa Jahmby kwa kupoteza kwao..

“Wewe, ulikuwa mtu mzuri na roho safi. Mpiganaji kwa ubora.  Saa hii ndio najua ulikuwa na jina innocent - ati Mary. On a light note, Ningekuwa na chance ingine moja tu nikuite Mary. Maria na nitumie vicheshi tofauti vya Mary juu yako. Nimalizie hivi, kama ilivyoandikwa mbele yangu, "Ndege anayeketi juu ya mti haogopi tawi kuvunjika, kwa sababu imani yake haiko kwenye tawi, bali kwenye mbawa zake," alisema.

Jahmby alipoteza maisha yake Jumatatu usiku alipokuwa akipokea matibabu katika Hospitali ya Nairobi. Alikuwa akipambana na ugonjwa wa endometriosis kwa miaka mingi.