"Nakiri sikuwa baba bora, nilikuangusha wakati ulinihitaji sana" - babake Jahmby Koikai ajuta

"Nimechelewa sana kujuta. Ninaweza tu kuishi na ukweli kwamba nilikuangusha wakati ulinihitaji sana, na sijivunii hata kidogo," babake Njambi alisema.

Muhtasari

•Babake Njambi alikiri kuwa anajilaumu kwa nyakati ambazo hawakuwa na maelewano mazuri, akibainisha kuwa alikosa nafasi za kurekebisha mambo kati yao.

•Alizungumza kuhusu kutokuwepo  katika maisha ya bintiye na kumwachia mzigo wa kumlea kwa mzazi mwenzake

amezungumzia uhusiano wake na marehemu binti yake, Jahmby Koikai.
Bw Daniel Koikai amezungumzia uhusiano wake na marehemu binti yake, Jahmby Koikai.
Image: HISANI

Bw Daniel Koikai, baba ya marehemu mtangazaji wa reggae Mary Njambi almaarufu Fyah Mummah Jahmby, amemuomboleza kwa ujumbe wa kihisia.

Katika ujumbe kwa bintiye ulionakiliwa katika ratiba ya ibada ya ukumbusho iliyofika Radio Jambo, Bw. Koikai alifunguka kuhusu kumbukumbu nzuri na mbaya zake yeye na bintiye.

Pia alifunguka kuhusu uhusiano wao ambao aliutaja kuwa mzuri na mbaya katika nyakati fulani.

“Kuhusu uhusiano wetu, tulikuwa na nyakati nzuri na mbaya. Nyakati zilipokuwa nzuri, tungeenda kununua bidhaa na kula chakula cha mchana katika baadhi ya mikahawa mjini, na ulifurahia mikutano hiyo kikamilifu. Nina’miss sana nyakati nzuri tulizoshiriki pamoja,” Bw Koikai alisema.

Babake Njambi alikiri kwamba anajilaumu sana kwa nyakati ambazo hawakuwa na maelewano mazuri, akibainisha kuwa alikosa nafasi za kurekebisha mambo kati yao.

"Wakati nyakati zilikuwa mbaya, tulikuwa tukienda kwa siku na miezi bila kuzungumza, jambo ambalo najilaumu na nitafanya kila wakati kwani nilipoteza nafasi ya kurekebisha mambo na wewe. Siku zote zitalemea sana moyo wangu,” alisema.

Katika ujumbe wake, Bw Koikai alikiri kwamba hakuwa baba bora kwa bintiye kila mara.

Alizungumza kuhusu kutokuwepo  katika maisha ya bintiye na kumwachia mzigo wa kumlea kwa mzazi mwenzake, na pia kutokuwepo kwa ajili yake wakati ambapo alikuwa akimhitaji zaidi.

"Ninakiri sikuwa baba mzuri na bora wakati wote kwako, na nilimwachia mama yako mzigo kwa hili. Matukio ambayo nilishindwa kwa njia nyingi kusimama nawe ulipokuwa ukipambana na ugonjwa wa endometriosis, najuta sana. Nimechelewa sana kujuta. Ninaweza tu kuishi na ukweli kwamba nilikuangusha wakati ulinihitaji sana, na sijivunii hata kidogo kwa mwenendo wangu,” alisema.

Siku ya Alhamisi, Juni 13, familia na marafiki wa marehemu Njambi walifanya ibada ya ukumbusho ya marehemu mtangazaji huyo wa reggae katika Nairobi Chapel, iliyo kwenye Barabara ya Ngong.

Mwili wake utazikwa leo, Ijumaa, Juni 14 katika Makaburi ya Lang’ata, Nairobi.