logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Niffer: Rafikiye Alikiba akamatwa kwa kuchangisha pesa kuwasaidia wahanga wa jumba lililoporomoka

Waziri mkuu Majaliwa alitoa amri ya kukamatwa kwake wakati alifanya ziara ya ghafla katika eneo la mkasa ambapo jengo la ghorofa 4 liliporomoka siku chache zilizopita.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Burudani19 November 2024 - 11:06

Muhtasari


  • Hii ni baada ya waziri mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa kutoa amri ya kukamatwa kwa mrembo huyo kwa kile alisema anachangisha hela za msaada bila utaratibu mwafaka.
  • Kwa mujibu wa sheria za Tanzania, mikasa kama ule wa Kariakoo upo chini ya wizara ya waziri mkuu, kitengo cha maafa.
  • Katika kitengo hicho, kuna sheria iliyopitishwa mwaka 2022 inayoratibu jinsi maafa kama hayo yanashughulikiwa.



MFANYIBIASHARA Niffer ambaye ni rafiki wa karibu wa msanii Alikiba ameripotiwa kutiwa mbaroni na jeshi la polisi Tanzania baada ya kudaiwa kuchangisha pesa za kuwasaidia wahanga wa jengo lililoporomoka Kariakoo sokoni.

Hii ni baada ya waziri mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa kutoa amri ya kukamatwa kwa mrembo huyo kwa kile alisema anachangisha hela za msaada bila utaratibu mwafaka.

Majaliwa alitoa amri ya kukamatwa kwake wakati alifanya ziara ya ghafla katika eneo la mkasa ambapo jengo la ghorofa 4 liliporomoka siku chache zilizopita.

“Yuko binti ambaye anaitwa Niffer, mumeona anasema anachangisha na nimeona mpaka jana alisema amekusanya zaidi ya milioni 37, atafutwe! Kwanza atuambie nani alimpa kibali cha kuchangisha. Utaratibu huu wa kuingiza pesa kwa simu yake alipata kibali wapi? Na amekusanya shilingi ngapi? Anasema ananunua maziwa, ameyapeleka wapi?” Waziri mkuu alihoji.

Waziri mkuu huyo alithibitishiwa kwamba Niffer tayari alikuwa amewekwa chini ya ulinzi na kuwataka kumhoji na kufunga ile akaunti aliyokuwa akitumia kuchangisha pesa.

Kiongozi huyo pia alitumia kisa cha Niffer kama mfano kutoa onyo kwa mwananchi yeyote wa taifa hilo dhidi ya kutumia fursa ya mkasa wa kuporomoka kwa jengo la Kariakoo kuchangisha pesa bila idhini ya mamlaka husika.

“Kwa kuwa mmeshampata, mhoji na mhakikishe kwamba mmefunga ile akaunti. Na kupitia tangazo hili, haturuhusu mtu yeyote kujitoa kusimamia michango ya watu kwa ajili ya hapa,” Majaliwa alisema.

Kwa mujibu wa sheria za Tanzania, mikasa kama ule wa Kariakoo upo chini ya wizara ya waziri mkuu, kitengo cha maafa. Katika kitengo hicho, kuna sheria iliyopitishwa mwaka 2022 inayoratibu jinsi maafa kama hayo yanashughulikiwa.

Wakili mmoja alieleza kwamba Niffer alifanya kosa chini ya kifungu namba 36(2) cha sheria hiyo ya maafa ambacho kinasema kwamba mtu yeyote atakayekusanya pesa za maafa bila kuwasilisha kwenye kamati ya maafa, atakuwa amefanya kosa na adhabu yake ni kifungo cha kati ya mwaka mmoja hadi miaka 5 jela au kulipa mara mbili ya fedha ambazo itabainika amezikusanya au yote mawili.



RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved