logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Muthoni Truphena: Mrembo Anayelenga Kuweka Rekodi Ya Kukumbatia Mti Kwa Saa 48

Mrembo huyo aliwakaribisha Wakenya wote kujitokeza kushuhudia akiweka rekodi hiyo ya dunia kwenye kitabu cha Guiness katika bustani ya Michuki.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Burudani02 February 2025 - 09:34

Muhtasari


  • "Nimekuwa nikitembea kwa muda mrefu kila asubuhi na jioni kwa wastani wa kilomita 42, hii imesaidia katika kuimarisha misuli yangu," aliongeza.
  • Pia amemshirikisha kocha wa yoga kwa ajili ya kujitayarisha kiakili.



MUTHONI Truphena, mrembo wa KENYA mwenye umri wa miaka 21 amewakaribisha Wakenya wote kushuhudia mchakato wake wa akilenga kuweka rekodi mpya ya dunia ya kukumbatia mti kwa saa 48 mfululizo.


Truphena, ambaye kupitia ukurasa wake wa Facebook anajitambulisha kama msanii na mwanaharakati wa masuala ya afya ya kiakili alisema analenga kuweka rekodi hiyo kwa kuitengua ile inayoshikiliwa na raia kutoka Ghana, Hakim Abdul.


“Leo ni siku ya hesabu. Kuanzia saa kumi na mbili jioni kwa saa za Kenya, nitaanza changamoto yangu ya kujaribu kukumbatia mti kwa saa 48 na kuzidisha rekodi ya sasa ya saa 24,” alisema Muthoni.


Mrembo huyo aliwakaribisha Wakenya wote kujitokeza kushuhudia akiweka rekodi hiyo ya dunia kwenye kitabu cha Guiness katika bustani ya Michuki.


Kulingana naye, uchaguzi wa Michuki Park ni wa kimkakati kwa sababu msukumo wake ulitoka kwa Waziri wa Mazingira wa wakati huo John Michuki ambaye alichangia pakubwa katika kubadilisha Mbuga hiyo na Mto Nairobi.


Bustani ya Michuki, ambayo zamani ilijulikana kama Mazingira Park, iko kando ya Mto Nairobi kutoka Globe Roundabout hadi Daraja la Makumbusho na ina upana wa eneo la takriban hekta 10.4.


Kwa mujibu wa jarida la People Daily, nia yake inalenga kutoa ufahamu juu ya umuhimu wa Asili katika kupambana na maswala ya afya ya akili ambayo anayataja kama janga nchini.


"Maswala ya afya ya akili yanaleta shida kati ya vijana na umma kwa ujumla, kwa bahati mbaya, watu hawathamini nguvu ya Mama Asili ya uponyaji. Ikiwa una msongo wa mawazo, tembea tu katika bustani ya jirani na ukute mti au ukae chini ya mti,” alinukuliwa na gazeti hilo.


Ili kufikia kuweka rekodi mpya, Muthoni amekuwa akifanya mazoezi kwa takriban miezi 5.


"Nimekuwa nikitembea kwa muda mrefu kila asubuhi na jioni kwa wastani wa kilomita 42, hii imesaidia katika kuimarisha misuli yangu," aliongeza.


Pia amemshirikisha kocha wa yoga kwa ajili ya kujitayarisha kiakili.


 


 


 



RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved