logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Mosiria: Waziri Wa Mazingira Nairobi Afumania Jamaa Na Mzoga Wa Paka Kwenye Begi

Mosiria alisema kwamba walimshika jamaa huyo akiwa na begi safi na baada ya kumsimamisha na kulichakura, walipigwa na butwaa kuona paka aliyekufa ndani.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Burudani21 February 2025 - 12:27

Muhtasari


  • Kupitia ukurasa wake wa Facebook, Mosiria alichapisha video akichakura begi ambalo alisema ni la jamaa ambaye walimkamata.
  • Waziri huyo alisema kwamba baada ya uchunguzi wa kina, walibaini kwamba huenda akawa mmoja wa wachuuzi wa mutura mitaani.

Geoffrey Mosiria

WAZIRI wa mazingira katika kaunti ya Nairobi, Geoffrey Mosiria ameibua tahadhari kwa wapenzi wa mutura ya kuuzwa mitaani baada ya kudai kumfumania jamaa akiwa na mzoga wa paka.

Kupitia ukurasa wake wa Facebook, Mosiria alichapisha video akichakura begi ambalo alisema ni la jamaa ambaye walimkamata.

Mosiria alisema kwamba walimshika jamaa huyo akiwa na begi safi na baada ya kumsimamisha na kulichakura, walipigwa na butwaa kuona paka aliyekufa ndani.

Waziri huyo alisema kwamba baada ya uchunguzi wa kina, walibaini kwamba huenda akawa mmoja wa wachuuzi wa mutura mitaani.

“Wakati wa usimamizi wa usafi usiku, nilitahadharishwa kuhusu mtu aliyekuwa amebeba paka aliyekufa, na mara moja, umati wa watu ambao walikuwa wamekusanyika walishuku kuwa anaweza kuwa mmoja wa wachuuzi wa mtura wanaodaiwa kutumia nyama ya paka kuandaa kitoweo hicho, wasiwasi uliochochewa na uvumi wa muda mrefu juu ya wauzaji wa vyakula wasio waaminifu kujihusisha na vitendo hivyo,” alisema.

Mosiria alitoa tahadhari kwa umma kuwa makini na vitoweo vya mutura wanavyokula na wachuuzi wanaowauzia, akisema kwamba baadhi wanatumia nyama isiyo halali.

“Ninawasihi kila mtu kuwa waangalifu zaidi kuhusu mahali anaponunua chakula cha mitaani. Ukiona chochote cha kutiliwa shaka, ripoti kwa mamlaka ili kusaidia kudumisha usalama wa chakula na kulinda afya ya umma,” aliongeza.

Waziri huyo amekuwa katika mstari wa mbele kusafisha jiji la Nairobi usiku na mchana huku akigongana vibega na wamiliki wa vilabu vya starehe, kanisa na wachafuzi wa mazingira.

 


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved