Baba Talisha atuzwa vinono kwa juhudi kubwa katika maandalizi ya mazishi ya Brian Chira

Baba Talisha ambaye alikuwa na urafiki wa karibu na marehemu Chira amehusika sana katika kuandaa mazishi yake.

Muhtasari

•Baba Talisha na binti yake wametuzwa kwa safari ya bila malipo ya Mombasa wakati wa likizo ya Pasaka.

•Kampuni hiyo ilibaini kuwa gharama zote za safari inayotolewa kwa tiktoker huyo na binti yake zimesimamiwa.

Image: INSTAGRAM// BABA TALISHA

Mtayarishaji wa maudhui mashuhuri wa Kenya Baba Talisha na binti yake wametuzwa kwa likizo bila malipo kutokana na juhudi zake kubwa katika kusimamia na kuratibu mazishi ya marehemu Brian Chira.

Kampuni ya utalii ya Expeditions Maasai Safaris, kupitia taarifa ya siku ya Jumatano ilimtunza mwanatiktok huyo na bintiye kwa safari ya bila malipo ya Mombasa wakati wa likizo ya Pasaka,  ikimtambua kwa usaidizi ambao ameipa familia ya Chira wakati wa majonzi.

Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo, Pancras Karema alimpongeza kwa juhudi ambazo aliweka katika kuhamasisha watu kwa lengo la kumpa marehemu Chira mazishi ya heshima, huku akibainisha kuwa hafla hiyo ya Jumanne ilikuwa ya mafanikio.

"Dhamira isiyobadilika ya Baba Talisha, uaminifu na uhisani umewalazimu mashabiki na wafuasi wetu kupendekeza zawadi kwa Baba Talisha kwa wema wake wa hali ya juu na wa kipekee. Hii inaendana na maono ya Expeditions Maasai Safaris ya kuheshimu na kuthamini waleta mabadiliko katika jamii,” Mkurugenzi Mtendaji wa Expeditions Maasai Safaris Pancras Karema alisema katika taarifa yake.

Aliongeza, “Ni furaha kubwa kwamba tunamzawadia Baba Talisha kwa bidii yake, na kujituma.”

Kampuni hiyo ilibaini kuwa gharama zote za safari inayotolewa kwa tiktoker huyo na binti yake zimesimamiwa.

Mtayarishaji wa maudhui ya Tiktok, Baba Talisha ambaye alikuwa na urafiki wa karibu sana na marehemu Brian Chira amehusika sana katika maandalizi ya mazishi yake katika kipindi cha siku kadhaa zilizopita. 

Amehusika sana katika kuratibu michango, kununua vitu vinavyohitajika, kutoa taarifa kuhusu maandalizi ya mazishi na hata kufariji familia.

Marehemu Brian Chira alizikwa siku ya Jumanne, Machi 26 nyumbani kwa nyanya yake katika eneo la Githunguri, Kaunti ya Kiambu.

Aliaga dunia mnamo Machi 16 baada ya kugongwa na lori katika barabara ya Kiambu.