Bahati amlalamikia mkewe Diana Marua kwa kudai marupurupu ya milioni 1.5 kila mwezi

Amedai kuwa tayari huwa anampa mke wake Diana Marua marupurupu ya kila mwezi ya Sh1milioni, ila hatosheki.

Muhtasari

•Msanii huyo mwenye umri wa miaka 31 alilalamika kuwa mama huyo wa watoto wake watatu bado hajaridhika na Sh1m anazompa.

•Diana alibainisha kuwa licha ya kuwa na kazi pia, ni wajibu wa mume wake kumpa pesa kwa matumizi yake binafsi.

Diana Marua na Bahati
Image: INSTAGRAM// DIANA MARUA

Mwimbaji Kelvin Kioko almaarufu Bahati amedai kuwa huwa anampa mke wake Diana Marua marupurupu ya kila mwezi ya Sh1milioni.

Katika chapisho kwenye Instagram, msanii huyo mwenye umri wa miaka 31 hata hivyo alilalamika kuwa mama huyo wa watoto wake watatu bado hajaridhika na kiasi hicho.

"Ninampa Diana Marua milioni 1 kama posho ya mke ya kila mwezi lakini anasema bado haitoshi. Kwani mnapewangwa ngapi?” Bahati aliandika.

Aliambatanisha chapisho lake na video ya Diana Marua akimkimbilia kwenye gari huku akidai posho yake ya kila mwezi mnamo Marchi 21.

“Babe, kwani huyu ameenda na hajaniachia posho ya mwezi? Babe, unaenda aje hivyo? Ni nini? Mbona unaenda na hujaniachia pesa? Posho ya kila mwezi?" Diana Marua alimlalamikia Bahati kwenye video hiyo.

Mama huyo wa watoto watatu alibainisha kuwa anahitaji pesa za kununua nywele, mapambo na mavazi.

Bahati hata hivyo alishangaa ni vipi kufikia Machi 22 mkewe alikuwa tayari amemaliza milioni moja aliyodai kumpa kwa mwezi huu.

“Babe milioni moja tu? Milioni moja tu? By the pandisha to 1.5 million, hiyo pesa ni kidogo babe. Nang’ang’ana, nafanyia bajeti, napunguza kitu na haitoshi,” Diana alisema.

Alibainisha kuwa licha ya kuwa na kazi pia, ni wajibu wa mume wake kumpa pesa kwa matumizi yake binafsi.

Bahati hata hivyo alimshauri kuchukua mkopo na kulipa baada ya kupokea posho yake ya kila mwezi mwanzoni mwa Aprili.