Ringtone Apoko ajigamba kuhusu kutumia shilingi milioni moja kununua T-shati moja

Muhtasari

•Ringtone amesisitiza kuwa utajiri wake na mali yake ya thamani hazijabadilisha uhusiano wake mzuri na Mungu.

•Mwanamuziki huyo ameshtumiwa mara nyingi kwa kutafuta kiki  kutumia mbinu tofauti ili kusalia maarufu katika tasnia ya muziki.

Ringtone Apoko
Ringtone Apoko
Image: HISANI

Mwimbaji wa nyimbo za injili mwenye utata mwingi Ringtone Apoko ameibua madai kuwa T-shati aliyonunua hivi majuzi imemgharimu shilingi milioni moja.

Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Ringtone amejigamba kuhusu kununua T-shati moja ya rangi nyeusi na nyeupe kwa bei ya gari zima kutokana na tajiri wake.

Mwanamuziki huyo aliyezingirwa na drama kochokocho amesisitiza kuwa utajiri wake na mali yake ya thamani hazijabadilisha uhusiano wake mzuri na Mungu.

"Nimevalia T-shati ya shilingi milioni moja. Hii T-shati ni milioni moja na bado nimeokoka. Bado nampenda Yesu. Wewe Mungu akaweza kukusaidia uweze kuvalia T-shati ya elfu tatu utaachana na mambo ya Mungu, ata simu hutakuwa unachukua za watu wa Mungu. Mimi nimenunua T-shati ya milioni moja na bado nampenda Mungu" Ringtone amesema kupitia kanda ya video aliyopakia Instagram.

Haya yanajiri wiki moja tu baada yake kudai kuwa alitumia shilingi laki moja kununulia binti ya mwanamuziki mwenzake Bahati, Heaven Bahati zawadi za siku ya kuzaliwa.

Mwenyekiti huyo wa kujitangaza wa muungano wa wanamuziki wa injili anajulikana kujipiga kifua mara mingi kuhusu utajiri wake mkubwa ambao umetiliwa shaka mara mingi.

Mwanamuziki huyo pia ameshtumiwa mara nyingi kwa kutafuta kiki  kutumia mbinu tofauti ili kusalia maarufu katika tasnia ya muziki.