"Sina mtoto mwingine!" Arrow Bwoy azungumzia madai ya kutema familia nyingine ili kuchumbia Nadia Mukami

Muhtasari

•Staa huyo alisema tayari alikuwa ametengana na mpenziwe kwa njia nzuri kabla ya kuzama kwenye mahusiano yake ya sasa

•Amefichua kuwa kabla ya kujitosa kwenye mahusiano na Nadia aliwahi kuchumbia takriban wanawake wengine wawili.

Image: INSTAGRAM// NADIA MUKAMI

Mwanamuziki Ali Yussuf almaarufu Arrow  Bwoy amepuuzilia mbali tetesi kuwa alimtema mkewe na watoto ili ajitose kwenye mahusiano na Nadia Mukami.

Alipokuwa anahutubia wanahabari wakati wa matayarisho ya uzinduzi wa Albamu yake, Arrow Bwoy alikiri kwamba alikuwa kwenye mahusiano mengine kabla ya kumchumbia Nadia.

Staa huyo alisema tayari alikuwa ametengana na mpenziwe kwa njia nzuri kabla ya kuzama kwenye mahusiano yake ya sasa. Aliweka wazi kuwa hakuwa amepata watoto wowote na aliyekuwa mpenziwe.

"Nilikuwa kwenye mahusiano lakini yaliisha. Ndio maana nikaingia kwenye mahusiano mengine. Kwa kawaida mimi nikiingia kwenye mahusiano nahakikisha huku kwingine kuko sawa kwanza. Nadia hajanipata kama sijaona dunia. Nimeona ndio lakini hayo ni mambo yaliyopita. Watu wamekuwa wakisema niko na watoto, mimi sina mtoto. Sina mtoto mwingine!," Arrow Bwoy alisema.

Mwanamuziki huyo pia alifichua kuwa kabla ya kujitosa kwenye mahusiano na Nadia aliwahi kuchumbia takriban wanawake wengine wawili.

"Sote tuko na historia. Wapenzi wangu wa zamani hawajapita wawili," Alisema.

Arrow Bwoy na Nadia waliweka mahusiano yao wazi mwaka uliopita. Iliwachukua wanamitandao muda mrefu kuyaamini mahusiano hayo kwani baadhi yao walidhani ni kiki.

Hivi majuzi wasanii hao wawili walitangaza ujauzito wa mtoto wao wa kwanza. Hapo awali walipoteza ujauzito mwingine.