"Sikutoka nje siku tatu, kunywa dawa tu!'" Harmonize afunguka jinsi kumkosa Kajala kumemwathiri

Muhtasari

•Harmonize alifichua kwamba ingawa amekuwa akifanya vizuri kimuziki, hajakuwa na raha maishani.

•Aliweka wazi kwamba hajalishwi na maneno ya watu kuhusu anachokifanya huku akieleza kuwa mhusika mwenyewe, Kajala anajua sio utani.

Harmonize na Frida Kajala
Harmonize na Frida Kajala
Image: HISANI

Nyota wa Bongo Rajab Abdul Kahali almaarufu kama Harmonize amesisitiza kwamba hafanyi utani na suala la kumtaka tena mwigizaji Fridah Kajala Masaja katika maisha yake.

Akihutubia waandishi wa habari siku ya Jumamosi, Harmonize alifichua kwamba ingawa amekuwa akifanya vizuri kimuziki, hajakuwa na raha maishani.

Harmonize alisema amekuwa akipitia kipindi kigumu tangu alipokosana na mwigizaji huyo mwaka jana na hata kuathirika kisaikolojia.

"Nimekuwa sawa, nimekuwa nikitengeneza muziki lakini kuna wakati nilisema sasa imezidi. Mimi sina raha. Mimi ni Harmonize, naweza kutumia umaarufu wangu kupata mwanamke mrembo zaidi kumliko, nimejaribu na kila mtu anajua. Lakini ilifika wakati nikasema namtaka yeye tena. Nataka kila mtu ajue hali ambayo nimekuwa nikipitia. Imekuwa mbaya, siku tatu sikutoka nje, nilikuwa nakunywa dawa tu. Imekuwa tatizo kwangu. Ni kitu ambacho nahisi ndani yangu," Harmonize alisema.

Mwanamuziki huyo aliweka wazi kwamba hajalishwi na maneno ya watu kuhusu anachokifanya huku akieleza kuwa mhusika mwenyewe, Kajala anajua sio utani.

"Mimi ni binadamu. Wakati mwingine nakosea. Mimi kama Harmonize hakuwezi kuwa na  sababu yangu kutokosea. Kuna wengi waliofanya makosa na kusamehewa. Nampenda sana, nataka arudi. Kila ninachokifanya naamini anajua kuwa ni kweli," Harmonize alisema.

Baba huyo wa mtoto mmoja ameeleza matumaini yake kwamba mambo yatakuwa sawa hivi karibuni huku akisema anaelewa kipindi anachopitia ni adhabu kwa mabaya aliyofanya.