Hatimaye Diamond amefunga ndoa na mpenzi wake wa siri kimya kimya

Muhtasari

• Watangazaji wa kituo cha redio cha Wasafi kinachomilikiwa naye Diamond Platnumz wanasema kwamba msanii huyo amefunga ndoa kimya kimya.

Msanii Diamond Platnumz
Msanii Diamond Platnumz
Image: screengrab: YouTube

Baada ya mamake Diamond, maam Dangote kuachia ujumbe kwenye Instagram yake uliokuwa unadokeza kwamba hatimaye baada ya kosa kosa mwanawe Diamond amepata mchumba, fununu zingine ambazo sasa zinasambaa kwenye mitandao ya kijamii ni kwamba msanii huyo tayari keshafunga ndoa chini ya maji.

Haya yaliwekwa wazi na mtangazaji wa kituo cha habari cha Wasafi, Lulu Diva ambaye alisema kwamba fununu za ndani kabisa na watu wa karibu na msanii huyo ni kwamba tayari ni mume wa mtu.

“Tetesi zinasema kwamba bosi wangu Diamond Platnumz sasa hivi ni mume wa mtu,” alisema Lulu katika video ambayo sasa hivi inatamba kwenye mtandao wa YouTube.

Lulu alisonga mbele kabisa hadi kumpigia simu mtangazaji mwenza Juma Lokole ambaye pia alihakiki kuwa ni kweli na kwamba mpaka alifika ofisini mwa Diamond na kumpata akiswali.

“Bosi kaoa tena mtoto mbichi, mtoto anajua dini vibaya mno Diva. Na uzuri bwana leo nimeingia ofisini kwake nimemkuta anaswali, nikasema Simba huyu huyu. Mtoto mbichi mzuri mkarimu anaongea vizuri, mtoto wa Kizanzibar” anasikika akisema Juma kwenye simu.

Ila kigugumizi kikubwa ni pale kwa kulitaja jina la ‘mke’ halali wa Diamond ambapo hakuna hata mmoja kati ya hao wala mamake Diamond ameliweka wazi jina lake.

Wengi wamekuwa wakishuku mpenzi huyo huenda atakuwa mwanamuziki mwenza Zuchu haswa ikizingatiwa kwamba Zuchu anatokea Zanzibar na Juma Lokole mwenyewe alidokeza kwamba mtoto mwenyewe ni wa Kizanzibar.

Juma alidokeza pia kwamba huenda Diamond atamtambulisha mpenziwe mpya kwenye mitandao ya kijamii na pia akasema kwamba mwezi mtukufu wa Ramadhani ukiisha tu hivi shughuli nzima ya sherehe ya harusi hiyo itafanyika.