Harmonize na Eric Omondi wafunguka ukweli kuhusu ugomvi wao

Muhtasari

•Wawili hao ambao wanajitambulisha kama mandugu walisema ni kawaida kwa wanafamilia kutofautiana.

•Eric alisisitiza kuwa ugomvi uliozuka hautaathiri undugu wake na Harmonize wala kudhalilisha uhusiano wa Kenya na Tanzania.

Image: INSTAGRAM// ERIC OMONDI

Mchekeshaji Eric Omondi na staa wa Bongo Harmonize wamesisitiza kuwa drama zilizoibuka kati yao wikendi hazikuwa kiki kama inavyodhaniwa na baadhi ya watu.

Wakihutubia waandishi wa habari, wawili hao ambao wanajitambulisha kama mandugu walisema ni kawaida kwa wanafamilia kutofautiana.

"Saa zingine ni kawaida kwa familia. Harmonize ni kaka yangu mdogo nami ni ndugu yake mkubwa, na hiyo ni kawaida ya familia," Eric Omondi alisema.

Mchekeshaji huyo alisisitiza kuwa ugomvi uliozuka hautaathiri undugu wake na Harmonize wala kudhalilisha uhusiano wa Kenya na Tanzania.

Harmonize kwa upande wake alikiri kuwa walikuwa wametofautiana na mchekeshaji. Aliweka wazi kuwa tayari wamesuluhisha mzozo wao.

"Eric ni ndugu yangu. Nampenda sana, amekuwa akinisapoti tangu siku ya kwanza. Kilichotokea ni kutofautiana tu. Yeye mwenyewe alikuja na kuniambia sisi ni mandugu na tulikosea. Sisi ni mandugu. Tumetokea mtaani, tunafanya kazi na tuko na talanta. Hiyo haiwezi kuvunja mahusiano yangu na mtu yeyote wa Kenya," Alisema Harmonize.

Mnamo usiku wa Ijumaa Eric Omondi na Harmonize wanaripotiwa kuhusika katika mzozo uliosababisha vita.

Baada ya tukio hilo Harmonize alitiwa mbaroni siku ya Jumamosi na kuachiliwa masaa machache baadae.

Jumamosi jioni wasanii hao wawili waliabiri ndege moja kutoka Nairobi hadi jijini Mombasa ambako walitumbuiza pamoja katika Club Volume.

Eric na Harmonize hata hivyo sio wageni kwa kiki. Wawili hao ni miongoni mwa wasanii maarufu ambao wanajulikana kufanya sarakasi mbalimbali katika juhudi za kukuza kazi zao.