•Harmonize ametangaza kuwa anatafuta mshirika ambaye yupo tayari kuwekeza naye huku akidai ni wengi wanaoisubiri bidhaa yake kwa hamu.
•Bosi huyo wa Konde Music Worldwide amefichua kuwa bidhaa yake itatambulika kama sigara ya Tembo.
Staa wa Bongo Harmonize ametuma ombi kwa mabwenyenye wa Tanzania kujitolea kushirikiana naye kufanikisha ndoto ya kuanzisha kampuni ya kutengeneza sigara.
Harmonize ametangaza kuwa anatafuta mshirika ambaye yupo tayari kuwekeza naye huku akidai ni wengi wanaoisubiri bidhaa yake kwa hamu.
"Nataka mtu ambaye atawekeza vizuri. Tufanye hili pamoja. Hakuna haja ya kufanya hili pekee yangu. Nahitaji ushirikiano mkubwa. Kila mtu anajua kiasi gani mtaa unasubiri hii kitu kwa hamu," Harmonize alitangaza siku ya Jumatano.
Bosi huyo wa Konde Music Worldwide amefichua kuwa bidhaa yake itatambulika kama sigara ya Tembo.
Amesema kuwa kampuni yake itatengeneza sigara kwa kutumia tubaku inayolimwa nchini Tanzania.
"Tembo cigarrette, tobako linalolimwa hapa hapa Tanzania!! Haya sasa matajiri waingie. Wachina sisi wenyewe tunaweza. Bei mtajipangia wenyewe wanangu," Alitangaza.
Mwanamuziki huyo amewataka washirika watakaovutiwa na pendekezo kuwasiliana na wasimamizi wake Chopa , Dkt Sebastian Ndege na Mohamed Mmari almaarufu Mjerumani.
Siku chache zilizopita Harmonize alidokeza kuhusu mpango wake wa kuanzisha Brand ya sigara. Aliwaomba mashabiki wake kupendekeza jina na muundo bora wa chapa ya sigara yake.
"Nahitaji jina zuri na muundo wa chapa yangu ya sigara maana kila chocho kila mtu anakohoa," Alisema kupitia Instagram.
Harmonize anajulikana kuwa mtumiaji wa sigara na mara nyingi amejionyesha hadharani akivuta bidhaa hiyo.