Penzi lataradadi huku Kajala akimpost Harmonize kwa mara ya kwanza tangu kurudiana kwao

Muhtasari

•Kwenye video hiyo Harmonize anaonekana akiwa amesimama kwenye gereji yake huku akiboroga maneno yasiyosikika.

•Takriban wiki moja iliyopita Kajala alizua hisia ya kurudiana kwao zaidi baada kujibu chapisho moja la bosi huyo wa Konde Music Worldwide kwenye Instagram. 

Harmonize na Kajala Masanja
Harmonize na Kajala Masanja
Image: HISANI

Mahaba ya wasanii wawili wa Tanzania Harmonize na Kajala Masanja yameonekana kuendelea kutaradadi kila uchao baada yao kurudiana.

Dalili kuwa wawili hao wametupilia mbali mzozo wao na tayari wamerudiana zilianza wiki kadhaa zilizopita wakati Kajala aliondoa block ambayo alikuwa amemwekea Harmonize kwenye Instagram.

Harmonize pia alianza kumtambua Kajala kama 'mke' wake katika chapisho zake za Instagram ambazo zilimlenga.

Takriban wiki moja iliyopita Kajala alizua hisia ya kurudiana kwao zaidi baada kujibu chapisho moja la bosi huyo wa Konde Music Worldwide kwenye Instagram. 

"🙏🏽🙏🏽🙏🏽❤️" Kajala aliandika chini ya chapisho la Harmonize ambapo alikuwa anampongeza kwa kusimama naye katika hali zote.

Kwa kipindi cha takriban wiki moja ambacho kimepita, wawili hao wamekuwa wakiacha jumbe tamu na makopakopa kwenye posti za kila mmoja wao.

Lakini leo hii (Jumatatu) Kajala amepiga hatua zaidi ambayo imemchukua zaidi ya mwaka mmoja. Muigizaji huyo amepakia video ya mpenzi huyo wake ambaye kwa sasa yupo nchini Uturuki.

Kwenye video hiyo Harmonize anaonekana akiwa amesimama kwenye gereji yake huku akiboroga maneno yasiyosikika.

"@harmonize💉😂" Kajala aliandika chini ya video hiyo ambayo alipakia kwenye Instastori zake.

Harmonize aliichapisha tena video hiyo kwenye ukurasa wake huku akimweleza mama huyo wa binti mmoja jinsi anavyompeza.

"Nimekumiss Anopama @kajalafrida," Aliandika.

Wasanii hao wawili hao walitengana Aprili mwaka jana huku ikidaiwa kuwa Harmonize alimtongoza binti ya Kajala, Paula.

Takriban miezi miwili iliyopita Harmonize alianzisha safari ya kujaribu kurejesha mahusiano yao. 

Miongoni mwa mambo ambayo alifanya ni kuomba msamaha hadharani, kununua zawadi ghali zikiwemo magari mawili aina ya Range Rover, kuchora tattoo ya muigizaji huyo na bintiye na kutundika bango la msamaha barabarani.