Mamake Diamond ashindwa kuzuia furaha baada ya Zuchu kumzawadia

Alhamisi wiki iliyopita Mama Dangote alitimiza miaka 54.

Muhtasari

•Diamond alimzawadi mamake Tsh20M huku Zuchu akiahidi kumnunulia zawadi wakati akitoka kwenye ziara yake.

•Vipondozi na manukato ni baadhi ya vitu ambavyo Mama Dangote alipokea kutoka kwa malkia huyo kutoka Zanzibar.

Mama Dangote na Zuchu
Image: INSTAGRAM

Mamake Diamond, Sanura Kassim almaarufu Mama Dangote ameendelea kupokea zawadi kochokocho hata baada ya siku ya kuadhimisha kuzaliwa kwake kupita.

Alhamisi wiki iliyopita alisherehekea miaka 54 tangu kuzaliwa kwake.

Huku akiadhimisha siku yake ya kuzaliwa Mama Dangote alichukua fursa kumshukuru Mola kwa kuzidi kumuweka hai.

"Kheri njema za siku ya kuzaliwa kwangu. Kibibi kizee kama anavyoniita Taraaj. Nashukuru Mungu kwa kuzidi kunipa pumzi mpaka hii leo," Aliandika kwenye ukurasa wake rasmi wa Instagram.

Mamia ya watu walimtakia kheri za siku ya kuzaliwa huku wanafamilia na watu wa karibu wakimwandalia karamu maalum.

Akiwa kwenye mahojiano na Wasafi Media, Mama Dangote alifichua kwamba alipanga kutumia siku hiyo nyumbani kwake.

"Nimeipokea siku hii freshi. Japo nilikuwa sijui kama kama karamu kama hii. Nashangaa niko nyumbani tu Esma ananiambia njoo tutoke, nafika hapa nakutana na vitu kama hivi. Sikujua nimefanyiwa karamu kama hii, nashukuru sana. Naona wanangu wananajali," Alisema katika karamu iliyoandaliwa kusherehekea siku yake ya kuzaliwa.

Baadhi ya wanafamilia na watu wengine wa karibu walijumuika naye kusherehekea siku hiyo maalum.

Mwanawe Diamond na Zuchu hata hivyo hawakuwepo kwani wakati huo walikuwa ziarani nje ya nchi Tanzania.

Diamond alimzawadi mamake Tsh20M huku Zuchu akiahidi kumnunulia zawadi wakati akitoka kwenye ziara yake.

"Zuchu alinipigia simu asubuhi akaniambia nitoke. Nilimwambia mimi sitoki nipo nyumbani. Aliniambia yupo Afrika Kusini kushoot video, akauliza aniletee zawadi gani. Nilimwambia chochote kile zawadi ni zawadi," Alisema.

Jumatatu mama huyo wa Diamond alionyesha vifurushi vya zawadi ambavyo alipokea kutoka kwa Zuchu.

Ingawa hakuonyesha zawadi zenyewe hasa ni nini, Mama Dangote aliashiria furaha yake kubwa baada ya kuzipokea.

"Zawadi za birthday zinaendelea lakini Zuhura . Asante Mama," Mama Dangote aliandika chini ya video ambayo ilionyesha vifurushi vya zawadi vilivyotumwa na Zuchu kutoka Afrika Kusini.

"Asante kipenzi changu Zuchu. Mzigo kutoka Afrika Kusini.. mama yake na mama Zuchu," Ujumbe wake mwingine ulisoma.

Vipondozi na manukato ni baadhi ya vitu ambavyo Mama Dangote alipokea kutoka kwa malkia huyo kutoka Zanzibar.