"Mpenzi wangu alivujisha video zangu za utupu baada ya kuachana" - Lulu Diva

Msanii huyo alisema hajui mwanaume huyo mpaka sasa ana video ngapi ambazo alimrekodi.

Muhtasari

• Katika mahojiano, Lulu Diva alisema mwanaume wake ambaye kwa sasa yupo Uingereza ndiye alivujisha video hizo chafu.

Lulu Diva
Lulu Diva
Image: INSTAGRAM

Mwanamuziki na muigizaji wa Bongo Fleva, Lulu Diva kwa mara ya kwanza kabisa amefunguka kuhusu Sakata la kuvujishwa kwa video za utupu wake wiki jana.

Akizungumza katika mahojiano ya simu na mtangazaji wa kituo kimoja nchini Tanzania, Lulu Diva amesema kwamba video hiyo ilivujishwa na aliyekuwa mwanaume wake ambaye kwa sasa anaishi nchini Uingereza.

Diva alieleza kwamba video hizo zilirekodiwa kitambo na mwanaume huyo aliamua kuzivujisha wiki jana baada ya Diva kutaka waachane ila mwanaume huyo akakataa na kupelekea kuvujishwa kwa video zile chafu kutokana na wivu wa kimapenzi.

Katika sauti hiyo ya mahojiano kwa njia ya simu, Diva anasikika akisema kwamba hakuwa anajua kwamba anarekodiwa na mwanaume huyo ambaye alikuwa anapenda sana mara nyingi kuongea na yeye kwa njia ya video ya mitandaoni.

“Nilikuwa naongea naye kimapenzi kama mpenzi wangu, ni mtu ambaye nilikuwa huru naye kwa sababu niliona ni kama mtu mzima. Kama sasa hivi nimebaki kujiuguza, lakini kama mwanaume ambaye nilikuwa naongea naye kama mpenzi wangu, unajua unaweza ukawa huru naye na kujiachia kama umetoka kuoga, ukawa uko wapi, hivo. Hata sijui hizo video anazo ngapi. Sijajirekodi mimi, amenirekodi yeye,” alisema Lulu baina ya kwikwi.

Wiki jana video chafu za msanii huyo zilitoboa tundu kwenye mitandao ya kijamii baada ya kuvujishwa na Mange Kimambi ambapo maneno mbali mbali yalizungumzwa huku baadhi waking’aka kwamba Diva amebugia sumu kutokana na aibu ambayo alijua fika itamkuta na wengine wakisema amelazwa kutokana na mshtuko wa moyo pindi baada ya Sakata lake kusagaa mitandaoni.