(+video) "Ukitaka kitu, sifu mtu! Hata malaika wanasifu Mungu na wana kila kitu" - Pst. Mgogo

Mchungaji alisema wenye wanajiona hawawezi kusifu mtu ili wapate wanachokitaka basi wazidi kukauka kwa mawe.

Muhtasari

 
• “Halafu wewe unasema eti siwezi kusifu mtu mimi, siwezi kupigia watu magoti. Endelea kula mawe kama unafikiria hii dunia uliiratibu wewe" - Mgogo.

Mchungaji Daniel Mgogo kutoka Tanzania anadai kwamba katika dunia hii ukijifanya huwezi kuwasifia watu haswa wakuu wako basi utazidi kuteseka na kula mawe.

Katika video moja ambayo imesambazwa kwenye mitandao ya kijamii, mchungaji Mgogo anaonekana akisema kwamba watu mbalimbali wamepandishwa vyeo na mamlaka duniani si tu kwa sababu wana akili na maarifa stahili bali ni kutokana na hulka ya kuwasifia wakubwa wao, akitolea mfano nchini Tanzania wale waliopewa vyeo serikalini baada ya kumsifia mama Samia Hassan.

“Kuna watu wamepandishwa vyeo, wamepewa ukuu wa mikoa, unafikiri walipewa kwa sababu wana akili nyingi? Wengi walipewa kwa sababu walianzisha kikundi cha kusifu.walikuwa wakimsifu mama sasa nchi iko kwenye mikono salama lakini baada ya kupewa vyeo, kimya!” Mchungaji Mgogo alisema.

Alisema kwamba kusifu hata kwa Mungu kuko kwani yeye ameketi kiti cha enzi anasifiwa usiku na mchana na Malaika hali ya kuwa wewe hapo hutaki kumsifu mtu ili upate unachotaka, basi utazidi kula mawe.

“Halafu wewe unasema eti siwezi kusifu mtu mimi, siwezi kupigia watu magoti. Endelea kula mawe kama unafikiria hii dunia uliiratibu wewe. Hii dunia imeratibiwa moja kwa moja kuna vitu huwezi ukavibadilisha. Vimewekwa kutoka juu Mungu mwenyewe anaketi katika sifa, Malaika wanafanya kazi ya kumsifu na wana kila kitu. Duniani hata hapa, unataka kula vizuri, sifu!” mchungaji Mgogo aliwashauri waumini wake.

Alisema kwamba yule ambaye hataki kusifu kwa kujiona afadhali basi azidi kukomaa hivo hivo na asiwahi nung’unika kwani bila kusifu mtu huwezi ukapata mkate wako wa kila siku.