Wakili Awataka Wanasiasa Kutokubali Matokeo, "Twende kortini Mtupatie kazi"

“Nusu ya idadi ya mawakili itamwakilisha Mlalamishi wa 3 katika Malalamiko husika na wengine wako katika jopo la IEBC. Kwa hivyo kwa kweli kuna kazi nyingi kwa kila mwanasheria,” Wakili Ochieng

Muhtasari

• "Sasa kukata rufaa ya matokeo ya uchaguzi ni kitu ya kunyima Wakili kwa kweli?" - Ochieng Oginga.

Wakili Anorld Oginga Ochieng akisikitika ni kwa nini wanasiasa wanakubali matokeo
Wakili Anorld Oginga Ochieng akisikitika ni kwa nini wanasiasa wanakubali matokeo
Image: Twitter//AnorldOginga

Wakili mmoja jijini Nairobi amezua utani katika mtandao wa Twitter baada ya kuwauliza wanasiasa mbona wanakubali kushindwa katika uchaguzi badala ya kuelekea mahakamani ili kuwapa mawakili hao kazi.

Anorld Oginga Ochieng ambaye ni wakili mchanga aliyependekezwa kuwania kitengo cha wakili mchanga zaidi mwaka 2021 aliwasihi wanasiasa kutokubali kushindwa kirahisi hivyo na badala yake kuelekea mahakamani kupinga matokeo ya uchaguzi na hivyo kuwapa mawakili kazi.

“Nusu ya idadi ya mawakili itamwakilisha Mlalamishi wa 3 katika Malalamiko husika na wengine wako katika jopo la IEBC. Kwa hivyo kwa kweli kuna kazi nyingi kwa kila mwanasheria,” Wakili Ochieng aliandika awali kwenye Twitter yake Jumanne.

Jumatano asubuhi baada ya matokeo kuanza kutolewa kutoka kituo kikuu cha kuhesabu kura Bomas, wanasiasa mbali mbali walionekana kukubali kwa urahisi kushindwa katika chaguzi hizo, jambo ambalo halikuenda vizuri kwa wakili Ochieng ambaye aliwataka kutokubali na kuwapa kazi ya kuwatetea mahakamani.

“Wanasiasa wapendwa…ACHENI kukubali kushindwa kirahisi hivyo, muache mchezo, twende MAHAKAMANI. Sasa kukata rufaa ya matokeo ya uchaguzi ni kitu ya kunyima Wakili kwa kweli??” Mwanasheria Ochieng Anorld alisaili.

Matamshi yake yanakuja huku wanasiasa wengi wakienda kinyume na destruri yao ya kawaida kwa kukubali haraka kushindwa katika chaguzi zilizofanyika jana.

Mwanasiasa wa kwanza kudokeza kuubali matokeo mapema usiku wa kuamkia Jumatano alikuwa mbunge wa Gatundu Kusini aliyeshindwa ugavana Kiambu, asubuhi kulipokucha wabunge kadhaa kama Nixon Korir wa Lang’ata, George Theuri wa Embakasi Magharibi, Amos Kimunya wa Kipipiri miongoni mwa wengine pia walitangaza kukubali matokeo na kuwapongeza washindani wao, licha ya kwamba tume huru ya uchaguzi na mipaka IEBC ingali bado kutoa tangazo rasmi kuhusu wagombea walioshindwa na wale walioshinda.