Mpelelezaji wa kibinafsi Jane Mugoh ameandikia pesa barua huku akitaka kujua ni kipi wakenya walizifanyia ili ziwakate kwa kiasi kikubwa na kuwaacha katika umaskini.
Kupitia ukurasa wake wa Facebook, Mugoh alilalama vikali kwa pesa huku akisema kwamba kama zinawakataa wengine basi yeye zimkubali tu kwa kujitetea kwamba yeye si mmoja wa wale waliosema kwamba pesa ndio mzizi wa maovu yote yanayofanyika katika kila sekunde iendayo kwa Mungu.
Katika ujumbe huo wa utani, Mugoh anasema kwamba watu wengi wanaogopa kuomba msamaha kwa pesa ili zirudi mifukoni mwao na kusema yeye ameamua kujitoa kimasomaso ili kuomba pesa msamaha kwa niaba ya kila mtu ambaye anaogopa kutaka radhi kwa Pesa.
Mpelelezi huyo aliyeshabikiwa sana kote ulimwenguni kutokana na ujasiri wake kupeleleza kesi za mauaji zingine zinazowahusisha watu mashuhuri weney pesa zao na hatari kubwa alichukua pia fursa hiyo kuwaambia mashabiki wake kwamba kwa sababu ya watu wote ambao wanawategemea basi wasije wakachoka kupambana katika maisha ili kutafuta pesa hata kama hazionekani.
"Jamani pesa, mimi si mmoja wa wale waliosema kwamba wewe ndio mzizi wa maovu yote. Watu wengi wanaogopa kukuomba msamaha. Rudi Uchumi unadorora. Naomba radhi kwa niaba ya watu wangu.. Wapendwa wafuatiliaji kwa sababu ya familia yako, Wapendwa, wategemezi hasa yatima, wagonjwa na wazee usikate tamaa. Mpendwa Mungu baadhi yetu tumewekeza kugawana mali zetu, kutoa kwa jumuiya, kutumikia nchi yetu. Tuna makovu kimwili na kiroho kupigana kwa ajili ya kukandamizwa," Mugoh alitia dua.
Mugoh alijaribu karata yake katika siasa ambapo alishiriki mchujo wa uwakilishi wa kike kaunti ya Kirinyaga kupitia chama cha UDA ila akabwagwa.